Nianzie wapi? – Nilinunua kitu mara ya kwanza kikafika kwa wakati (ndani ya siku 15) bila chenga, mara pili – mizunguo kibao ilichukua zaidi ya siku 20…ya tatu..bado nusu iwe magumashi..ila tayari nimelipia bidhaa zingine tena! 🙂 Huu ni mtazamo wangu juu ya huduma ya app ya KiKuu!
Watu wengi sana wanatamani kuwa na imani na ununuzi wa vitu kutoka mtandaoni, lakini changamoto zipo kadhaa;
- Kuwapa watu taarifa zako za kibenki wakati ata huwafahamu
- Mzigo kutokufika, nitaanza kumshika shati nani?
Ingawa kununua vitu nje mara nyingi kunakuwa nafuu kibei kulinganisha na kama ukinunua kitu hicho hicho kwenye duka la karibu lakini changamoto hizo mbili ni kubwa na za ukweli kabisa. Nishasikia stori nyingi za watu kujaribu kununua vitu mtandaoni na kutowafikia nchini. Changamoto hizi ndizo ambazo app ya KiKuu inajaribu kuzikabili.
Kupitia huduma yao utaweza kununua bidhaa mbalimbali kuanzia mavazi, vitu vya jikoni, elektoniki n.k, vyote vipo katika bei ya Tsh na pia unaweza lipia kwa kutumia huduma za malipo ya simu kama M-Pesa, Airtel Money n.k. Bei zake zote zinajumuhisha gharama za usafirishaji wa bidhaa. Pia wana ofisi yao hapa hapa Dar es Salaam, inasemekana ipo Kariakoo, sijawahi fika bado.
> Aina ya Vitu wanavyouza
Wanajitahidi kuongeza ongeza bidhaa katika app yao lakini bado huduma kama za Kaymu na Jumia zina bidhaa nyingi sana hasa kwenye eneo la vifaa vya elektroniki ukilinganisha na KiKuu. Ila kwenye masuala ya mavazi na mambo mengine kama hayo bado KiKuu wapo vizuri tuu.
Vitu unavyoweza kununua kwenye app ya KiKuu – Mavazi ya kiume/kike, Mabegi,Viatu, Vifaa vya elektroniki,Vitu vya chumbani/jikoni/bustanini na michezo, Saa na vitu vingine vya urembo, Midoli na vitu vingine vya watoto.
> Jinsi app hii inavyofanya kazi
Kwanza huduma ya KiKuu inapatikana kupitia app tuu na si kwenye njia ya mtandao, wana app kwa ajili ya Android na pia kwa ajili ya iOS (iPhone).
Unapoona bidhaa na kuichagua kununua utapewa maelekezo ya kulipia kupitia mfumo wa Airtel Money, Tigo Pesa au M-Pesa. Usipolipia bidhaa husika ndani ya siku saba basi wanaifuta katika oda zako na hivyo itabidi ununue upya.
Kupitia app hii unaweza kupata taarifa zote muhimu (track) kuhusu mzigo wako kuanzia unapotoka China hadi unapofika hapa Dar, na ata unapoletewa. Kuna wastani wa siku 10 hadi 15 wewe kupata bidhaa yako kuanzia siku uliyoilipia.
> Nilichopenda
Urahisi wa kuangalia bidhaa katika makundi mbalimbali kupitia app yao. Nishajaribu huduma nyingi za ununuaji mtandaoni kwa Tanzania lakini ni app hii tuu ndio nimefanikiwa kuitumia sana. Njia ya kulipia ni rahisi, na unapewa hatua kwa hatua.
Kama kitu hujakipenda unaweza kurudisha ndani ya siku chache (7) baada ya mzigo kukufikia, ila inabidi uhakikishe bado hujakitumia kitu hicho na ukirudishe kwenye hali ya kama ulivyokipokea.
Pia kwenye baadhi ya bidhaa kama watu walikwishanunua unaweza kuta maoni yao wakisema walipata bidhaa hiyo katika hali gani, hili linaweza kukusaidia kujua kama ununue au vipi.
> Ambacho sijafurahishwa nacho (Panaitaji Maboresho)
Kwa sasa nishanunua vitu vilivyonifikia vitatu lakini ni cha kwanza tuu ndio kilikuja bila usumbufu wowote. Mzigo wangu wa pili ulipelekwa sehemu sizo wakati mleta mzigo alinipigia siku moja kabla kuniuliza aniletee wapi mzigo wangu. Hali hii ilisababisha niupate siku zaidi ya 20 tokea niagize wakati kawaida huwa uchukua siku 10- 15.
Huduma kwa wateja wamezubaa. Kuna umuhimu sana wa kuwa na mtu shupavu na anayejali kutatua tatizo la mteja. Ni vizuri KiKuu kuwa na namba ambayo una uhakika wa kupiga na kusikilizwa lakini mtu niliyokuwa nakutana naye nikipiga simu hakuwa anajali kunitatulia tatizo langu kwa haraka. Matokeo yake nilikuwa ni mimi hadi nimtafute na mara zote naanza kuulizwa maswali yale yale badala ya yeye kunipa taarifa kama ameshughulikia tatizo la ucheleweshwaji wa mzigo wangu.
Mtu anayesambaza mizigo pia anatakiwa ajipange vizuri. Bidhaa yangu ya kwanza kununua ingawa alinipigia simu siku moja kabla bado alipeleka sehemu siyo na hivyo kusababisha mimi kuweza kupata kitu hicho siku nyingi baadae. Mzigo wa tatu kununua alikuwa ameubeba akaja ofisi hiyo hiyo kuleta mzigo wa mtu mwingine lakini akaondoka na mzigo wangu bila kunitaarifa, kumpigia simu akiwa tayari mbali kidogo ndio akagundua ana mzigo wangu pia. Hivyo ina maanisha hajipangi vizuri kujua vitu alivyovibeba na ni wapi anavipeleka – awe na kitabu cha kuweka vema (ku’tick’) pale anapofikisha vitu.
Nje ya hapo app ya KiKuu ni huduma nzuri sana. Napenda ofa wanazoziweka za hadi kufikia ata mapunguzo ya asilimia 85% kwenye baadhi ya bidhaa karibia kila siku. Kwa watu ambao hatupendi kwenda kudhurula kwenye maduka au kuingia na kuzunguka Kariakoo basi app hii inasaidia sana. Na pia kupitia ofa zake unaweza jikuta unanunua kitu kwa bei nafuu sana ukilinganisha na gharama za kama ungeenda dukani.
Je wewe ushawahi kutumia huduma hii au nyingine yeyote ya mtandaoni katika kufanya manunuzi? Tuambie mtazamo wako katika ulichokutana nacho.. 🙂
Download/Pakua – KiKuu Google PlayStore | KiKuu iOS