Mtandao wa LinkedIn ambao ndiyo mtandao wenye mafanikio makubwa katika kitengo cha taaluma umeingia katika vichwa vya habari vya mitandao mbalimbali baada ya kufikia makubaliano na kampuni ya Microsoft ambayo katika makubaliano hayo itanunua hisa za LinkedIn kwa jumla ya dola za kimarekani bilioni 26.2.
Katika dili hili LinkedIn wataendelea kufanya kazi kwa uhuru kama ambavyo wanafanya kwa sasa, hii ina maana kwamba mtandao huu hautabadili taratibu za uendeshaji wake tofauti na mitandao mingi ambayo hubadilisha mtindo wa ufanyaji wa kazi pindi inaponunuliwa.
Mtandao wa LinkedIn ni mtandao wa kijamii unaowasaidia watu kutengeneza ‘urafiki’ na kufahamiana na wengine hasa kwenye masuala ya ajira. Ni moja ya mtandao unaotumiwa na wengi katika kukamilisha masuala ya kikazi na kibiashara.
Mtandao huu umekuwa unakua kwa kasi na kutawala vyema katika kitengo cha mitandao ya kitaaluma, hivi karibuni mtandao huu ulifanya mabadilko kadha wa kadha ambayo kimsingi yaliwavutia wateja wengi wapya pamoja na kuwafanya wateja wa zamani kurudi na kuanza kuutumia tena.
Mabadiliko ambayo yalifanywa na mtandao huu yameifanya LinkedIn iwe na mtandao mkubwa wa watu wenye taaluma mbalimbali hivyo umekuwa unapata wawekezaji wengi ambao kwa namna fulani wamefanya mtandao huu kuwa imara zaidi.
Baada ya dili hili mkurugenzi mtendaji wa mtandao huu atakuwa anaripoti moja kwa moja kwa bosi mkuu wa Microsoft Satya Nadella, zaidi ya hayo mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi wa mtandao huo ameunga mkono dili hili.