Wanasayansi katika Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine nchini Tanzania wanapanga kuwatuma panya waliopokea mafunzo kwenda kutumiwa kugundua kifua kikuu nchi za nje.
Panya hao ambao awali walitumiwa kugundua mabomu yaliyoachwa chini ya ardhi, kwa miaka kadha sasa wamekuwa wakitumiwa kugundua watu wanaougua kifua kikuu sana katika magereza na viwandani.
Panya hao, ambao kiteknolojia hujulikana kama panya wa SUA-APOPO, wamebainika kuwa hugundua visa vya maambukizi ya kifua kikuu haraka na kwa ufasaha.
Panya hao hudaiwa kuwa na uwezo wa kupima sampuli 140 za makohozi kwa dakika 15 tu, wakati mtaalamu wa maabara aliyebobea huweza kupima wagonjwa 25 kwa siku.
Awali panya hao walitumiwa Tanzania na Msumbiji pekee lakini sasa chuo kikuu hicho kinapanga kuwapeleka Ethiopia na Bangladesh wakatumiwe huko. Ethiopia ni moja ya nchi zilizotatizwa zaidi na aina ya vijidudu vya kifua kikuu visivyosikia dawa.
Kwa mujibu wagazeti la Daily News la Tanzania Bi. Mariam Juma (mmoja wa wanasayansi katika chuo hicho) amenukuliwa akisema kwamba kutafunguliwa kituo cha utafiti jijini Dar Es Salaam. Mtafiti huyo aliongeza na kusema kuwa maafisa pia watawahimiza watu kujipima kujua hali yao.
Je, unadhani hatua hiyo ya panya hao kutumika kwa ajili ya utafiti kwingineko barani Afrika kutafanya Tanzania izidi kujulikana na kuzidi kutanua sekta ya Sayansi? Tuambie katika comment. Soma makala mbalimbali kupitia Teknokona.
Chanzo: BBC, All Africa