Facebook Messenger nao wameamua kufanya kama walivyofanya WhatsApp mapema mwaka huu kwa kufanya mazungumzo ya watu kuwa salama zaidi (end-to-end encryption).
Katika hali ya kufanya mazungumzo kati ya mtu na mtu kwenye Facebook Messenger kuwa salama zaidi wameamua kuja na ‘feature’ mpya waliyoiita ujumbe wa siri (Secret messages). Hatua hii itasaidia mazungumzo baina ya mtu na mtu kuwa ni vigumu kudukuliwa.
Kwa kawaida ujumbe mfupi wa maneno ambao huwa tunatumiana kupitia mitandao ya kijamii au mitandao ya simu, n.k huifadhiwa kwenye kompyuta yenye kasi na uwezo wa hali ya juu wa kuhifadhi data(severs).
Facebook Messenger wameamua kukifanya kinamaanisha kuwa jumbe hizo zitakuwa hazifadhiwi tena kwenye severs bali anayetuma/kupokea ujumbe huo ndio watakuwa na wanausoma na si mtu mwingine yoyote (‘end-to-end’ encryption kwa lugha ya kimombo).
Mbali na hilo mtu anaweza akaficha ujumbe aliotuma baada ya ujumbe huo kupokelewa kwa kuweka muda fulani ambao ujumbe huo utakuwa hauonekani kwenye mazungumzo(chats) yenu. Muda huo ni kati ya sekunde 5 mpaka saa 24.
Hatua hii ya Facebook Messenger kufanyiwa maboresho ya kutoweza kusoma ujumbe wa mtu haiwafurahishi watu wote ikiwemo serikali kwani kwa hatua hii haitaweza kufuatilia jumbe za watu kwenye Facebook Messenger na hivyo kuwa kikwazo kwao hivyo hivyo kwa wadukuzi pia, hawataweza kudukua taarifa kutoka kwenye app hiyo.
Maboresho hayo bado yapo katika hatua za majaribio kwani hivi sasa ni baadhi ya makundi tu ndio wenye wamepewa uwezo wa kujaribu maboresho hayo mapya lakini maboresho hayo yanatarajiwa kupatikana kwa watu wote kati ya mwezi wa 8 au 9.
Nini maoni yako kuhusu maboresho hayo yaliyofanya kwenye FB Messenger? Tuandikie hapo chini katika sehemu ya maoni. Endelea kusoma makala mbalimbali kupitia TeknoKona.
Vyanzo: Tech Times, Neurogadget