Kampuni binafsi nchini Marekani imepata ruhusa kutoka serikali ya Marekani kufanya biashara ya safari za kwenda kwenye mwezi.
Kampuni hiyo ya nchini Marekani inategemea kuweza kutoa safari kwa watu na mashirika/makampuni.
Moja ya lengo lao ni pamoja na kuweza kuona kama wanaweza jihusisha na utafiti wa kuvuna rasilimali zilizopo katika ardhi ya mwezi.
Kampuni inafahamika kwa jina la Moon Express (kwa kifupi MoonEx) na wanategemea kufanya safari ya kwanza kwenda mwezini mwishoni mwa mwaka 2017.
Ujio wa kampuni hii unazidi kuonesha jinsi gani makampuni binafsi yanazidi kuwekeza katika teknolojia za kurahisisha safari za anga za juu na nje ya dunia. Hii ni baada ya mafanikio makubwa yaliyofikiwa na kampuni zingine binafsi kama vile SpaceX na Virgin Galactic.
Kampuni ya MoonEx inategemea pia kushinda zawadi ya dau la dola milioni 20 za Kimarekani kutoka Google. Google wana shindano la ‘Lunar XPRIZE’ ambapo kushinda pesa hizo kampuni binafsi inatakiwa kufikisha kifaa kwenye ardhi ya mwezi kisha kuondoka tena na kifaa hicho hicho kutua tena umbali wa takribani futi 1,500 kutoka kilipokuwa mwanzo…pia kifaa hicho kinatakiwa kutuma video na picha za ubora wa kiwango cha HD huku duniani.
Inasemekana lengo la MoonEx ni kufikia muda ambao mtu ataenda ofisini kwao na kusema ‘Ningependa kusafiri kwenda kwenye Mwezi na kurudi siku flani’ na wao wakakujibu ‘Hakuna tatizo, jaza fomu hii’..kwa sasa hakuna sehemu ambapo jambo hilo linawezekana.
Una mtazamo gani juu ya harakati za kampuni ya MoonEx?
Vyanzo: Mitandao mbalimbali