Hivi karibuni kumekuwa na ukuaji wa umaarufu wa apps na huduma zinginezo za vivinjari zinazozuhia matangazo ya mtandaoni.
Ukuaji wa watu wengi kutumia huduma za namna hii kumefanya Facebook na mitandao mingine inayotegemea mapato kupitia matangazo ya mtandaoni kuathirika kimapato. Facebook wametangaza uboreshwaji katika huduma zao za matangazo na pia wamesema wameboresha mfumo wao ili kuweza kuzishinda apps na huduma zingine zinazoficha matangazo (ad blocking).
Inasemakana kuna takribani watumiaji milioni 200 wa kompyuta wanaotumia huduma za kuzuia matangazo, na pia kuna wengine milioni 420 wanaotumia huduma ya kuzuia matangazo kwenye simu janja zao.
> Kuhusu maboresho ya matangazo
Facebook wamesema wamefanya maboresho na kuwapa watumiaji uhuru zaidi katika kuchagua aina ya matangazo yatakayokuwa yanasukumwa kwao.
Facebook wamedai ya kwamba wamefanya uchunguzi kwa watumiaji wake na wamegundua sababu kubwa ya watu wengi kutopenda matangazo ya mtandao huo ni suala zima la kuletewa matangazo ambayo wao wanaona hayawahusu au hayahusu mambo wanayoyapenda.
> Kuhusu vita dhidi ya apps na huduma za kuzuia matangazo
Kwa tovuti na mitandao ya kijamii inayotegemea mapato yake kupitia tovuti zake ukuaji mkubwa wa utumiaji wa huduma za kuzuia na kuficha kabisa matangazo zimeathiri sana mapato yao.
Kuhusu hili Facebook wameboresha mtandao wao kufanya iwe vigumu zaidi kwa apps na huduma za kuzuia matangazo kuweza kutofautisha kati ya matangazo na ‘post’ za kawaida. Hili litaathiri jinsi mifumo ya kuzuia matangazo inavyofanya kazi na hivyo kuweza kushinda kuyafahamu matangazo.
Je una mtazamo gani juu ya matangazo ya kimtandao? Je unadhani yanakusaidia kivyovyote?
Vyanzo: Facebook na The Forbes.