Instagram ndio mtandao wa kijamii maarufu sana unaojihusisha na maswala ya picha kwa ujumla. Hili ni jambo jema kwani mpaka sasa mtandao huo wa kijamii umeshushwa mara bilioni 1*.
Hii ni namba kubwa sana — kwa Instagram — na kingine kinachofanya namba hii nizidi kuiona kubwa ni kwamba taarifa hizi ni kutoka Google PlayStore tuu. Kwa maneno mengine ni kwamba hapo bado hujajumlisha na wale wa App Store na Market Place na masoko mengine mengi ya App za simu janja.
Instagram ilianzishwa mwaka 2010 na tangia ianzishwe iliweza kupata mafanikio makubwa na ya haraka, kwa kipindi cha miezi mitatu tuu ilifanikiwa kupata watumiaji milioni 1. Hiyo haikutosha baada ya mwaka ikapata watumiaji milioni 10.
Mwanzoni ilikua ikitumika kwa vifaa vya iOS tuu lakini baada ya muda kampuni ikajiweka karibu kwa watumiaji wa Android na baadae hata kwa simu janja zinazotumia programu endeshaji nyingine.
Instagram ni moja katika ya App chache (ya 19 mpaka sasa) katika zile chache ambazo zimeshushwa mara bilioni na zaidi katika soko la Google Play Store.
Kwa Facebook, Instagram ni App ya nne kushushwa mara bilioni katika soko la Google Play Store na hiyo ni baada ya Facebook App, WhatsApp na Facebook Messenger App kuwa wa kwanza kufikisha namba hiyo.
Cha kushangaza hapa ni kwamba japokuwa App hiyo imeshushwa zaidi ya mara bilioni moja katika Google Play Store bado Instagram ina watumiaji walio’Active milioni 500. Hii inamaanisha kuwa wengi waliokuwa wanashusha App hiyo ni wale wale (labda wanashusha katika vifaa vingine).
Ni pongezi kubwa kwa kufikiwa kwa hatua hiyo na Instagram, fikiria bilioni moja katika Google Play Store. Pengine tukijumuisha na masoko mengine tunaweza hata tukapata bilioni mbili au zaidi.