Kama unamiliki iPhone 6s ambayo inajizima pindi inapofikia 30% ya chaji na ulikuwa bado hauelewi tatizo ni nini basi taarifa hii inakuhusu.
iPhone tayari wamekubali kwamba baadhi ya simu ambazo wamezitengeneza zinashida katika battery zake na wanawashauri watumiaji wa simu ambazo zinamatatizo kuzirudisha ili ziweze kurekebishwa.
Tatizo ni nini katika hasa!?
Baadhi ya wamiliki wa iPhone 6s wameripoti simu zao kuzima zikifikia 30% ya chaji katika betri, tatizo hili ambalo limejitokeza kwa baadhi ya simu hizi linapelekea simu kuzima kama vile imeishiwa chaji kabisa na ili kuweza kuiwasha tena simu basi unahitaji kuichomeka simu katika chaja yake tena.
Kama simu yako ina tatizo hili ufanye nini?!
Inategemea hasa na wapi ambapo ulinunua hiyo simu yako, kama unaweza kwenda na kuiripoti ulipoinunua basi ni vyema na ni rahisi zaidi wao watakusaidia cha kufanya. Kama uliinunua nje ya nchi ama uliiagiza nje ya nchi na huwezi kuirudisha kwa upesi basi unaweza kufungua ukurasa huu wa Apple ambao umejikita kuwasaidia wahanga wa tatizo hili katika mitandao.
Kama unairudisha simu yako basi ni lazima kwanza uizime huduma ya Find my iPhone, lazima uizime na ufute taarifa zako zote katika simu, na iwapo simu yako ilivunjika kioo basi utatakiwa kugharamia kwanza gharama za kubadilisha kioo kilichovunjika kwa kuwa kubadilisha betri ni lazima kioo kiwe kizima.
Apple wanasema tatizo hili lipo kwa simu chache sana na hasa zilizotengenezwa kati ya mwezi Septemba na Oktoba mwaka 2015, wao wanadai kwamba tukio hili sio kubwa sana na halihatarishi usalama kwa kuwa ni bidhaa chache tu ndizo ambazo zimeathirika.