Katika suala zima la teknolojia katika miaka ya hivi karibuni neno ‘selfie’ si geni kwa wengi na ni moja ya vitu vilivyotokea kupendwa na watumiaji wengi wa simu janja.
Katika hali ya kusukitisha vijana kadhaa huko New Delhi-India wamepoteza maisha baada ya kugongwa na treni walipokuwa wakipiga picha kwa kutumia kamera ya mbele yaani selfie.
Kundi la vijana lilikwenda katika kituo cha reli kupiga selfie mbele ya treni zilizokuwa zinawadia lakini wawili kati ya vijana hao walichelewa kuondoka katika reli hiyo na treni ikawakanyaga.
Wakati wa kupiga picha, waliiona treni ikija wakasogea pembeni lakini treni nyingine ilitokezea upande wa pili na walikwama katikati. Waligongwa na mojawapo ya treni hizo.
Kamera iliyokuwa ikitumika katika tukio hilo imepatikana kutoka kwa vijana. Kwenye kamera hiyo zimekutwa picha na picha jongefu yaani video, video bado inafanyiwa uchunguzi ingawa picha hizo zinathibitisha kuwa walikuwa wanaruka kutoka reli moja hadi nyengine.
Mwaka uliopita vijana wawili walipoteza maisha baada ya kuzama kwenye mto uliokuwa na maji mengi walipokuwa wakipiga selfie. TeknoKona tunashauri kuchukua tahadhari pale tunapokuwa tunapiga picha za selfie.
Kumbuka kusambaza makala na pia kuungana nasi kupitia Facebook, Twitter, Instagram, YouTube, Telegram na Google Plus
Chanzo: BBC