Inaonekana sera ya Rais mpya wa Marekani, Bwana Donald Trump ya kulazimisha makampuni yanayotegemea soko la Marekani kutengeneza bidhaa hizo nchini humo inaanza kufanya kazi.
Samsung wameingia kwenye orodha ya makampuni kadhaa ambayo yameanza kujitathmini na kuandaa mikakati ya kuwekeza katika viwanda nchini Marekani. Rais huyo wa Marekani ameshasema lengo lake moja ni kuongeza kodi kwa bidhaa zinazotoka nje, akilazimisha makampuni mengi yawekeze Marekani ili kutengeneza ajira kwa wananchi wake.
Chanzo kimoja kutoka makao makuu ya Samsung kimevujisha habari ya uamuzi huo na kusema tayari maandalizi yanafanyika kuona ni jinsi gani na kwa bidhaa gani viwanda vingine vijengwe nchini Marekani.
Samsung ni moja ya kampuni kubwa na muhimu sana kwa uchumi wa Korea Kusini. Pato la Samsung huwa linachangia kati ya asilimia 17 hadi 20 ya pato la taifa la Korea Kusini.
Pia kampuni nyingine kutoka Korea Kusini, LG nayo ilikwishatangaza mwanzoni mwa mwaka huu ya kwamba ingawa inapinga sera za Bwana Trump ila nao pia watawekeza katika viwanda nchini Marekani ndani ya kipindi cha mwaka huu.
Sera za Rais Trump zimeathiri makampuni mengi katika eneo la Teknolojia hasa hasa kwenye suala la kutegemea viwanda vya nje ya nchini hiyo na pia kwenye uwezo wa kuajiri wafanyakazi kutoka nje ya nchi – hasa kwa nchi ambazo Trump ametoa sheria kali za kuzuia watu hao kuingia nchini humo kwa sababu za kigaidi.
Je una maoni gani na njia hii ya kuongeza viwanda katika nchi ili kukuza ajira?
Kumbuka kusambaza makala na pia kuungana nasi kupitia Facebook, Twitter, Instagram, YouTube, Telegram na Google Plus
Chanzo: Fortune na tovuti mbalimbali