Apple wataka simu zao ziwe na uwezo wa kikompyuta kamili, tena kompyuta mpakato. Kampuni hiyo nguli katika eneo la simu janja kupitia programu endeshaji ya iOS imechukua hakimiliki ya teknolojia ya kufanikisha hilo.
Tayari makampuni mengi yamekuwa na wazo la namna hili kama vile kampuni ya Canonical, ambao ni watengenezaji wa programu endeshaji ya Ubuntu OS. Ila baada ya miaka kadhaa ya kujikita na utengenezaji na uboreshwaji wa simu zinazotumia Ubuntu OS na zitakazoweza kugeuka kompyuta nzima pale zitakapochomekwa na Monitor (TV n.k) kingine, wametangaza kuachana na wazo hilo tena.
Pia kupitia toleo la simu la Samsung Galaxy S8 mtumiaji ataweza kuiunganisha na monitor (tv n.k) pamoja na keyboard na kipanya kupitia teknolojia ya bluetooth na programu endeshaji ya kwenye simu hiyo itafunguka hadi kupitia monitor na atatumia kama kompyuta.
Wazo la Apple ni la kitofauti kidogo. Teknolojia waliyoichukulia hakimiliki ni uwepo wa kompyuta mpakato (laptop) ambayo inasehemu ya kupachika simu ya iPhone na programu eneshaji hiyo ya simu itafunguka kama OS kamili kwenye laptop hiyo.
Na simu itakapo kaa ndio itatumika pia kama kipanya cha laptop hiyo (trackpad). Kikubwa hapa ni kwamba kama kikompyuta mpakato hicho kikiuzwa kwa bei nafuu kabisa kwa sababu teknolojia nyingi itakuwa tayari ipo kwenye simu basi itahakikisha kumpunguzia gharama mtu – Badala ya kununua simu yenye uwezo mkubwa na pia kutumia pesa nyingine nyingi kwenye laptop.
Ila hii sio teknolojia iliyochukuliwa hakimiliki, pia mafaili yanaonesha kuna nyingine ambayo pia ipo katika mfumo wa laptop ila eneo la kioo (display) mtu atapachika tablet ya iPad.
Wengi hawaamini kama tunaweza kuona bidhaa muda wowote hivi karibuni, inawezekana ikawa bado Apple wanaangalia na kuchunguza kama wanaweza kuja na bidhaa ya kitofauti.
Ila pia tusishangae kama moja wapo, hasa hasa hii inayotegemea simu kuja kuwa bidhaa kamili siku moja.
Vipi wewe una mtazamo gani juu ya wazo la teknolojia hii.?
Chanzo: Engadget