Ndege inayotumia nishati ya jua imetua mjini Cairo, Misri na kupokelewa na waziri na maafisa wengine wa ngazi ya juu wa maswala ya usafiri wa anga wa nchi hiyo.
Ndege hiyo ilikuwa imefanya safari ya saa 48 kutoka mji wa Seville-Uhispania mapema wiki hii. Haikutumia mafuta ya ndege ya kawaida hata chembe bali nguvu za kawi zinazotokana na miale ya jua(solar energy).
Ndege hiyo inaongozwa na marubani wawili wa Uswizi huku kituo cha mwisho cha safari hiyo ya majaribio kikiwa Abu Dhabi. Saa chache kabla ya kutua mjini Cairo ndiyo ilikuwa na changamoto zaidi kwani kwa mara ya kwanza betri ya ndege hiyo ilikuwa imeshuka hadi asilimia 30 pekee.
Haijajulikana mkondo huo utachukua muda gani kwani itategemea zaidi hali ya hewa mpaka Umoja wa Milki za Kiarabu ambapo ndipo mpango huo wa majaribio wa ndege hiyo ya solar ulianza hapo mwaka 2015.
Awali marubani hao wawili walikuwa wakifanyakazi katika mradi wa sola uitwao ‘Solar Impulse’ kwa muda wa zaidi ya miaka 10.
Japo ni safari ya polepole ndege hiyo imeweza kuvuka anga zaidi ya nchi 7 nyinginezo zikiwa ni zile zilizo na shughuli nyingi za ndege za usafiri wa umma. Ni mradi ambao kufikia sasa umegharimu $100 millioni, tangu 2002 lakini lengo la utafiti huu ni kuwa huenda hatimaye gharama kama hiyo itakuwa ndogo ikilinganishwa na gharama ya harakati za kukabiliana na changamoto za kuongezeka kwa hali ya uchafuzi wa hewa.
Ndege hiyo inasifiwa na wengi kwani inapunguza uchafuzi wa mazingira kwa kiasi kikubwa kutokana na kutumia nishati ya Jua pia inaweza kuweka rekodi kwani ina uwezo wa kuruka mita 8,500 juu ya bahari na kwenda kasi kati ya 55-100Kph.
Kwa hakika ndege hii italeta mapinduzi makubwa katika sekta ya usafirishaji wa anga itakapoanza kazi rasmi. TeknoKona tutazidi kukuhabarisha juu ya ndege hii.
Vyanzo: BBC, Reuters