Sayansi ya uzazi inazidi kuwa na mapya kila leo jambo linalopelekea kuleta matumaini katika utatuzi wa changamoto mbalimbali ambazo sekta ya afya na sayansi ya uzazi inakumbananazo.
Kuna wale watoto wanaozaliwa kabla ya muda wao (kabla ya miezi tisa) jambo ambalo linasababisha wazaliwe huku baadhi ya viungo vyao vikiwa bado havijakamilika ipasavyo na hivyo kuwekwa kwenye chombo maalum (incubator) ambacho joto lake ni sawa na joto la kwenye tumbo la uzazi.
Wanasayansi nchini Marekani wamebuni tumbo bandia la kutengeneza ambalo katika siku zijazo linaweza kutumiwa kuwekea watoto wanaozaliwa kabla ya muda wao, maarufu kama njiti.
Watafiti katika hospitali ya watoto ya Philadephia wanasema lengo lao ni kuweka mazingira ambayo watoto wanaozaliwa kabla muda wao kutimia wanaweza kukuza viungo vyao vya mwilini kama vile mapafu na viungo vyengine.
Kutokana na kwamba watoto wanazaliwa wakiwa njiti na uangalizi wao ni wa hali ya juu sana sitakuwa nimekosea nikisema kuwa sayansi ya kuhifadhi watoto kwenye tumbo la bandia itasaidia sana na hata kuokoa vifo vya watoto. Kifaa hicho kimetengezwa kwa kutumia mfuko wa plastiki, uliojazwa maji ya kutengeza yanayoigiza mazingira ya tumbo la uzazi.
Wanasayansi wanaamini mfuko huo unaweza kuwa tayari kwa majaribio ya binadamu baada ya miaka mitatu mpaka mitano kuanzia sasa.
Vyanzo: BBC, The Verge