Google imekuwa kampuni ya kwanza ya nje kuzindua huduma nchini Cuba na kuongeza matumaini ya mageuzi katika nchi hiyo iliyojitenga kwa muda mrefu.
Kituo kikubwa kimefunguliwa cha uhifadhi wa data ambacho kitatumika kama hifadhi ya taarifa za video za Youtube. Cuba inaendelea kufungua milango ya upatikanaji wa habari kwa wanachi wake ambao kwa kipindi kirefu hawakuwa wakipata.
Mpaka sasa huduma ya Intaneti nchini Cuba imekuwa ikipatikana kwa kebo(Cable) kupitia chini ya bahari kutoka nchi ya Venezuela ambayo kasi yake ni ndogo sana.
Lakini kwa sasa seva za Google zitakuwa na uwezo wa kuhifadhi data nchini humo na hivyo kuharakisha kasi ya Intaneti. Google ilitangaza mpango huu mwishoni mwa mwaka jana kwa wananchi wa Cuba kwa kuwaambia waCuba watarajie maboresho makubwa ya huduma na kuwapunguzia muda wa kusubiri muda mrefu video za Youtube kufunguka.
Hii ni hatua kubwa kwa wananchi wa Cuba ambao serikali yake imekuwa ikidhibiti matumizi ya Intaneti.
Hata hivyo waCuba wanaotumia huduma za Intaneti ni wachache sana kutokana na miundo mbinu duni ya upatikanaji wa huduma hiyo pamoja na udhibiti wa Serikali.
Watu wengi hawajapewa ruhusa ya kuwa na huduma ya Intaneti majumbani kwao na wanaweza kutumia huduma hiyo katika maeneo ya kazi, taasisi za elimu na katika maeneo ya umma 240 yaliyowekwa Wi-Fi.Katika maeneo ya umma ambayo kuna Wi-Fi mwananchi anatakiwa alipie Dola 1.50 (Sawa na Shilingi 3,350 ) kwa saa na katika Intaneti cafe gharama ya kupata huduma ya Intaneti ni Dola 4.50 (Sawa na Shilingi 10,000) kwa saa.
Gharama hizo ni kubwa mno kwa mwananchi wa Cuba kwa kuwa wastani wa mshahara kwa mwezi ni Dola 25. Takwimu zinaonesha ni asilimia 5 tu ya watu wa Cuba wanaopata huduma ya Intaneti.