Kama umeona matatizo kwenye Whatsapp jana Jumatano usiku, hali hiyo haikuwa yako pekee, bali kwa mamilioni ya watu duniani kote.
Huduma ya WhatsApp haikuwa ikipatikana kabisa kwa watumiaji wengi ndani ya uingereza, Ulaya na maeneo mengi Duniani kwa zaidi ya masaa mawili. Tatizo la kukosa huduma ya WhatsApp lilianza saa tatu usiku mpaka saa Tano na Nusu usiku.
Miji ya London, Manchester, Leeds, Paris, Munich, Milan, Berlin, Vienna pamoja na sehemu kubwa ya Uholanzi ilikuwa ya kwanza kuripotiwa kutopata huduma za WhatsApp.
Sehemu zingine zilizoripotiwa kutopata huduma za Whatsapp ni Afrika Kusini, Amerika ya Kusini, Mexico na Marekani.
Haikuwezekana kutuma meseji wala kupokea hatua iliyopelekea watu wengi kupatwa na sintofahamu. Kila aliyejaribu kutuma meseji alikuwa akiambiwa “connecting”.
Wengi walikimbilia Twitter kuripoti tatizo hilo la kukosa huduma ya kutuma na kupokea meseji. Tatizo hilo bado haijajulikana nini hasa kilichosababisha.
Msemaji wa WhatsApp alisema, “Baadhi ya watu walipatwa na tatizo la kupata huduma ya WhatsApp kwa kipindi kifupi leo(Jana). Tunafanya kazi ya kurejesha huduma kwa asilimia 100 kwa kila mtu na tunaomba msamaha kwa usumbufu huo”.
Baada ya masaa zaidi ya mawili, iliripotiwa hali ya huduma ya WhatsApp kurudi kama kawaida kwa watumiaji wake.