Mwanaume mmoja nchini Aljeria afunguliwa mashtaka na kufungwa baada ya kumnin’giniza mtoto ghorofani ili kupata Likes za Facebook.
Mwanaume huyo ambaye ni ndugu wa mtoto huyo ameshtakiwa kwenda jela miaka miwili kwa kosa la kuweka uhai wa mtoto huyo hatarini.
Ilikuwaje?
Mwanaume huyo alipost picha inayoonesha ameshikilia mtoto huyo kihatari – kwa kushika shati tuu, huku mtoto huyo akiwa anatazama chini kutoka kwenye jengo lefu la ghorofa. Vyombo vya habari vya nchini humo vimesema walikuwa katika ghorofa la 15.
Kwenye post hiyo ya Facebook aliandika maneno ‘1,000 likes or I will drop him’ – yaani ‘ Nipate Likes 1,000 au vinginevyo nitamuachia’.
Watumiaji mbalimbali wa mtandao huo wa kijamii wali’share post hiyo na vyombo vya usalama vya nchini wakilalamika kuhusu tukio hilo.
Kwenye kesi mwanaume alijitetea akisema eti watumiaji wa mtandao wamechezea picha hiyo, hakumshikilia eneo la hatari bali walikuwa kibarazani na kulikuwa na vyuma vya usalama mbele ya mtoto huyo na anahisi watumiaji wa mtandao walifuta vyuma hivyo katika picha iliyosambaza kwenda kwenye vyombo vya usalama.
Ata hivyo hakufanikiwa katika utetezi huo kwani hakuna picha yoyote aliyoweza kuionesha kutetea alichokiongea.
Ingawa baba wa mtoto huyo alishauri asamehewe na aachwe huru bado mahakama ikampa kifungo cha miaka miwili.