Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) imepiga marufuku urushwaji angani wa vifaa vya kieletroniki visivyo na rubani (drones) Tanzania bila kupata kibali maalum kutoka mamlaka hiyo na Wizara ya Ulinzi na Usalama.
Katika taarifa yao rasmi iliyotolewa kwenye vyombo vya habari na kutiwa sahihi na Mkurugenzi Mkuu wa TCAA, Hamza Johari, imefafanua kuwa uendeshaji wa shughuli zote za anga nchini uko chini ya Mamlaka ya TCAA kwa mujibu wa sheria na kanuni zilizopo.
Taarifa hiyo imesema “Ifahamike kuwa kuanzia sasa, taasisi au mtu binafsi anayetaka kununua, kufanya majaribio au kurusha angani vifaa hivyo visivyotumia rubani anapaswa kupata idhidi ya Wizara ya Ulinzi na Usalama pamoja na kibali kutoka TCAA,”
Utumiaji wa vyombo vya drones umekuwa maarufu sana duniani kote na tayari utumiaji wake ulianza kukua nchini pia. Drones zinatumika kwa ajili ya upimaji ardhi, upigaji picha za mnato na za video.
Maeneo makuu ambayo utumiaji wa drones umekua kwa kasi nchini ni pamoja na uchukuaji wa video za muziki (kuchukua picha za juu). Si hao tuu bali ata kwenye matukuo ya makusanyiko ya watu wengi wapiga picha wengi walianza kutumia drones, kama unakumbuka picha za mnato na video za kipindi cha uchaguzi uliopita mara nyingi drones zilitumika kuonesha wingi wa watu katika mikutano husika.
Je hii haitaleta changomoto ya urasimu katika sekta ya ubunifu (innovation) na utumiaji binafsi?
Kwanza ni muhimu kufahamu ya kwamba tayari inasemekana kulikuwa na utumiaji mbovu wa drones zinazobeba kamera hasa hasa katika kurekodi maeneo yasiyotakiwa. – hii inaweza kwa kutoheshimu faragha za wengine au kuingia maeneo ya vyombo vya usalama.
Swala la kuwa na sheria na vibali vinavyosimamia utumiaji wa drones ni muhimu sana, ila kwa kiasi kikubwa nadhani utaratibu mzima utawafanya watumiaji wa kawaida wa majumbani kukatishwa tamaa kabisa na utumiaji wa drones katika maeneo yao.
Utaratibu wa kupata kibali ata kwa mtumiaji mdogo wa nyumbani kwake wa kumtaka aende TCAA na pia Wizara ya Ulinzi na Usalama ni mkubwa sana.
Tukumbuke utumiaji wa drones nchini kwetu bado mdogo, tuone jinsi taifa kubwa kama la Marekani lenye watumiaji wengi zaidi wa ndege za bila rubani wameziwekaje sheria zake.
- Kwanza sheria na taratibu, zinapatikana na kusomeka kwa urahisi kwenye mtandao wa mamlaka ya anga ya nchini humo
- Kwa mtumiaji wa drones wa nyumbani na mwenye drones yenye chini ya uzito wa gramu 249 haitaji kwenda kujiandikisha popote ili kuweza kutumia drone yake.
- Na kama drone yake imezidi uzito huo basi anachotakiwa kufanya ni kuandikisha drone yake kupitia tovuti ya mamlaka hiyo. – hapa inamaanisha wameondoa ugumu wa urasimu (bureaucracy) kwa mtumiaji huyu mdogo.
Ila bado mtumiaji huyu amepewa utaratibu wa kufuata katika utumiaji wake, ambapo asipozingatia basi anaweza shitakiwa. Hii ni pamoja na kutorusha drones hizo juu ya eneo lenye watu, kutorusha eneo la makazi ya mwingine, kutorusha ndani ya umbali kadhaa kutoka maeneo yenye viwanja vya ndege na taratibu zingine ndogo za kuzingatia.
Ila kwa watumiaji wa drones kwa masuala ya kibiashara na tafiti basi wao ndio wana taratibu ndefu za kufuata zinazohusisha usajili na upatikanaji wa leseni. Kama kimombo kimekukaa vizuri basi unaweza soma zaidi kuhusu sheria na taratibu za utumiaji wa drones nchini Marekani hapa -> FAA.GOV
Tunategemea utaratibu huu mpya utaweza kufungua milango ya mitazamo mingine mbalimbali na huko mbeleni tuweze kuboresha zaidi na hivyo kuondoa ugumu kwa watumiaji wa kawaida kushindwa kunufaika na utumiaji wa drones kisa tuu hofa ya urasimu mzima wa kupitia ili kufanikiwa kupata vibali. Iwe rahisi ata kwa wakazi wa miji midogo kabisa mikoani kuweza kutumia bidhaa inayofurahiwa na wengine wengi duniani kote.
One Comment
Comments are closed.