Kama ambavyo tumekuwa tukieleza sana katika mfululizo wa taarifa zetu hapa Teknokona kwamba kwa sasa maisha bila ya kuwa na simu ya mkononi ni kama jambo lisilo wezekana.
Katika hali kama hiyo, wengine hulazimisha kuwa na simu hata katika maeneo yasiyo ruhusiwa kisheria kumiliki simu. Miongoni mwa maeneo ambayo hayaruhusiwi kumiliki simu ni kwa wafungwa au watuhumiwa waliowekwa katika magereza.
Simu za mkononi zipatazo 13,000 zimekamatwa katika jela mbalimbali nchini Uingereza kwa mwaka jana. Katibu wa Haki, David Lidington alitoa taarifa kwa waziri wa magereza hiyo wakati akielezea matatizo yanayokabiliwa na magereza nchini humo ikiwemo usalama duni kwa wafungwa na matumizi ya madawa ya kulevya.
Alisema ukamataji wa simu hizo pamoja na Line 7,000 za simu umesaidia kuzuia kuendelea kupanga uhalifu zaidi kwa wafungwa.
Mpango wa kuwekeza Paundi milioni mbili katika Teknolojia ya kuchunguza simu na mbwa 300 wenye mafunzo maalumu ya kukamata madawa ya kulevya imesaidia kukamata visivyotakiwa kuwa ndani ya jela hizo. Katika zoezi hilo pia kulikamatwa kilo 225 za madawa ya kulevya.
Tatizo la kuingizwa simu katika magereza sio lipo Uingereza tu, hata Tanzania limeelezwa kuwa lipo.
Mwaka 2015, Mkuu wa Magereza Mkoa wa Dar es Salaam kamishna Joel Bukuku, wakati akihojiwa na baadhi ya waandishi wa habari ofisini kwake katika hitimisho la ziara yao ya kutembelea magereza kadhaa mikoani kwa lengo la kujifunza utekelezaji wa programu ya urekebishaji wafungwa kupitia miradi inayoendeshwa na jeshi hilo alikiri kuwepo kwa tatizo kama hilo.
Amesema ni kosa kwa mfungwa kuingiza simu gerezani na kwamba wanapowabaini hatua kali zinachukuliwa pamoja na askari jela wanaokuwa wameshirikiana nao.
“Ni kweli simu zinaingizwa magerezani na wafungwa kwa kificho au kwa kula njama na askari wasiokuwa waadilifu. Hili ni kosa kwa mujibu wa sheria zetu za magereza, hivyo tunapobaini hatua kali zinachukuliwa kwa aliyehusika.
“Hili ni suala ambalo linafanyika kwa kificho sana. Kwa mfano mdogo tu, hivi karibuni kuna mfungwa wa kike tulimbaini ameficha simu kwenye sehemu zake za siri (ukeni) hadi tukalazimika kumpatia huduma ya kumlaza kuweza kuitoa,” amesema.
Kamishna Bukuku ameongeza kuwa pamoja na usiri huo unaotumika, bado wameendelea kupiga vita hali hiyo kwa kuwaeleimisha wafungwa kujiepusha na vitu visivyoruhusiwa kuingizwa magerezani.
Ingawa bado jitihada zinaendelea kudhibiti uingizwaji wa simu katika magereza lakini hali hiyo bado ipo kwa wafungwa kupenyezewa simu huko huko magerezani.
Pamoja na udhibiti huo na adhabu mbalimbali kwa wanaokamatwa na simu magerezani, bado watu wameendelea kutumia simu katika magereza.
Je ni kweli kwa maisha ya sasa ni ngumu mtu kuishi bila ya kutumia simu ya mkononi?