Bitcoin ambayo ni pesa ya kidigitali imepata pigo baada baadhi ya wadau waliokuwa wanaiunga mkono kutofautiana na kupelekea baadhi ya wadau hao kuanzisha pesa nyingine ya kidigitali inayoitwa Bitcoin Cash.
Ingawa mpasuko huu haujasababisha kushuka kwa thamani ya Bitcoin kwa kiasi kikubwa lakini kumesababisha sintofahamu kwa wadau wake ambao hawajaamua kama wanataka kujiunga na kundi lililojitoa ama waendelee kubaki na Bitcoin.
Kwa ambao hawaijui Bitcoin:
Bitcoin ni mfumo ama utaratibu wa malipo ambao ni wa kidigitali na usiomilikiwa wala kuratibiwa na benki ama serikali. Katika mfumo huu malipo yanafanyika kati ya mtumiaji na mtumiaji mwingine bila ya kupitia mtu wa kati(benki).
Pesa hii ambayo inathamani kubwa ( bitcoin moja ni sawa na karibu milioni 6 za kitanzania) hutumika kununua bidhaa mbalimbali na pia kama malipo ya huduma mbalimbali na wapo ambao wanahifadhi pesa hii kama uwekezaji kwa kuwa imekuwa ikipanda thamani yake.
Mfumo huu hauna mamlaka maalumu kwaajiri ya kuuratibu na kuumiliki hivyo unaratibiwa na yeyote mwenye uwezo hasa hasa wadau wanao utumia.
Wadau wa bitcoin walitofautiana katika namna ambayo mfumo huu unatakiwa uendeshwe, jambo hili likapelekea moja kati ya makundi mawili yaliyotofautiana kuamua kuanzisha mfumo mpya ambao wameuita Bitcoin cash.
Mpasuko huu tayari umeishaanza kuleta vurugu katika sekta ya pesa za kidigitali baada ya kampuni maarufu kwa uratibu wa mauzo ya bitcoin inayojulikana kama Coinbase kutishiwa kupelekwa mahakamani baada ya kukataa kujihusisha na pesa mpya ya Bitcoin Cash.
Kwa wote ambao wanavutiwa na uwekezaji wa aina hii ama wanavutiwa kufanya biashara kwa kutumia pesa za kidigitali basi ni muhimu wakapata ushauri kutoka kwa watalamu wa uchumi hasa pesa za kidigitali katika kipindi hiki ambapo bado haijajulikana mpasuko huu utakuwa na madhara gani kwa Bitcoin ambayo ndiyo pesa ya kidigitali yenye nguvu zaidi.