Kampuni ya televisheni ya kulipia ya China StarTimes inapanga kuzindua huduma za matangazo ya TV ya kidijitali bila malipo kwenye sehemu za vijijini barani Afrika, ikiwa ni sehemu ya majukumu yake ya kijamii.
Mkurugenzi Masoko na Uhusiano wa kampuni hiyo nchini kenya Bw. Japheth Akhulia amesema mradi huo utanufaisha vijiji 10,000 barani Afrika.
Amesema Lengo ni kuunganisha huduma za kidijitali za televisheni ambapo vijiji vingi vya Afrika haviwezi kupata huduma za televisheni.
Huduma hii itahusisha upatikanaji wa bure wa chaneli cha TV za bure zinazopatikana katika nchi husika, hii kwa Tanzania ni kama vile TBC na zingine nyingi.
Utoaji huduma hiyo unafuatia mradi wa majaribio uliofanikiwa ambapo kampuni hiyo ya China iliunganishia kaya 100 kusini magharibi mwa Kaunti ya Kajiado nchini Kenya.
“kwa bahati mbaya wananchi wengi wa vijijini hawawezi kumudu gharama za kununua Ving’amuzi kwa ajili ya kuangalia televisheni, Kwa hiyo tumeamua kusaidia vijiji vya Afrika kufaidika na faida inayopatikana Startimes katika kutoa huduma zake kwa wananchi”, alisema Akhulia.