Kampuni ya Samsung inaweza kupata uchungu wa kibiashara kutoka kwa mteja wake mkubwa wa vioo wa Apple baada ya kuelezwa ana mpango wa kutumia vioo vinavyozalishwa na kampuni ya LG.
Kwa muda mrefu vioo vya simu vinavyotumika kwenye simu za iPhone vimekuwa vikitengenezwa na Samsung vikiwemo vya OLED vilivyotumika katika simu za iPhone X.
Vioo vya OLED vimekuwa vikiuzwa kwa bei kubwa kiasi cha kusababisha gharama simu kuwa mkubwa; simu rununu inayotumia kioo cha aina hiyo kuanzia $1,000 na kuendelea.
Apple imeanza mazungumzo na kampuni ya LG kwa ajili ya kununua vioo vya OLED ambapo watanunua kwa bei nafuu zaidi kuliko Samsung. Chanzo cha habari kinasema LG itaanza kuwauzia Apple vioo kuanzia milioni 2 mpaka 4 kwa awamu ya kwanza.
Ingawa LG inataka kuwa mtoa huduma mkuu wa Apple lakini kwa sasa haitawezekana mpaka itakapoimarisha zaidi uzalishaji wake wa vioo hivyo vya OLED. Kwa muktadha huo Apple italazimika kununua na vioo vya Samsung ili kukidhi uzalishaji wa simu zake.
Inaelezwa kwa Apple kuanza kununua vioo kwa LG itafanya bei ya vioo hivyo kupungua kidogo kwa sababu ya ushindani wa kibiashara na hivyo kupungua bei kwa baadhi ya simu mpya zitakazotumia vioo vya OLED kutoka LG.