Apple ipo katika mpango wa kutengeneza kila kipuli kinachotumika kujenga iPhone. Kwa muda mrefu sasa kampuni hiyo imekuwa ikifanya kila wanaloweza kujaribu kuhakikisha wanatengeneza vipuli vyote muhimu vinavyotumika katika ujenzi wa simu ya iPhone.
Katika ripoti iliyotolewa na mtandao wa bloomberg, inaonesha tayari Apple wapo katika hatua nzuri katika lengo lao la kutengeneza screen/display zao kwa ajili ya matumizi ya kwenye bidhaa zao kama vile iPhone.
Kwa miaka mingi Samsung ndio amekuwa mtengenezaji mkubwa zaidi wa screen zote zinazotumika kwenye simu mbalimbali hii ikiwa ni pamoja na zinazotumika kwenye simu za iPhone. Hii imekuwa ikimaanisha kwa kila simu ya iPhone inayouzwa bado Samsung pia amekuwa akinufaika kimapato.
Ripoti ya Bloomberg inaonesha ya kwamba Apple wametengeneza kiwanda cha utengenezaji wa display/screen katika jimbo la California. Kiwanda hicho kitakuwa kinatengeneza screen za teknolojia mpya inayokwenda kwa jina la MicroLED, kwa sasa bado teknolojia hii haitumiki.
Hadi sasa Apple wamekuwa wanatumia display/screen za teknolojia ya OLED ambazo wanazipata kutoka kwenye viwanda vya Samsung, ila ubaya wake ni kwamba bado Samsung anabakia na haki ya kutumia na kuwauzia wengine display za teknolojia hiyo. Mfano simu zake nyingi za kisasa kama vile Samsung Galaxy S9 nazo zinakuja na teknolojia hiyo.
Kwenye masuala ya prosesa tayari Apple alishaacha kununua kutoka kwa wengine, wanatengeneza prosesa zao wenyewe. Hili linahakikisha prosesa hizo zinatengenezwa kwa ukaribu zaidi na utendaji kazi wa programu endeshaji yake – iOS, hii uhakikisha ufanisi bora zaidi wa simu.
Kwenye kiwanda hicho cha utengenezaji wa MicroLED tayari Apple wameajiri zaidi ya wahandisi 300. Display za MicroLED zinasemekana zitakuwa bora zaidi ya OLED, zitaonesha rangi kwa ubora zaidi.
Chanzo: Bloomberg