Kwa mara ya kwanza kampuni ya utengenezaji wa simu ya Apple ambayo ndiyo inatengeneza simu maarufu za iPhone imeaanza kuziuza simu ambazo zilirudishwa na wateja ambao hawakuridhika nazo.
Kabla ya leo Apple ilikuwa ikiyatumia makampuni mengine kuuza simu walizozifanyia matengenezo baada ya kurudishwa kwa shida mbalimbali.
Kwa wateja wa Apple ambao wamenunua simu za kampuni hiyo hupewa muda wa siku 14 baada ya kununua simu na kama hawataridhishwa na utendaji kazi wa simu hizi basi wanaweza kurudisha simu kwa Apple, simu hizi baada ya kurudishwa hapo nyuma zilikuwa zinatengenezwa kubadili betri na kava za nje kisha kuuzwa kwa makampuni ambayo baadaye huziuza.
Apple wameamua kuanza kuziuza wao wenyewe simu hizo ambazo zimefanyiwa marekebisho pamoja na kujaribiwa kuona kwamba zinafaa kwa matumizi, simu hizi zinauzwa kwa bei ya chini ukilinganisha na bei ya simu mpya kama hizo kitu ambacho kinazifanya ziwavutie wapenzi wa simu ambao mifuko yao imepigwa na ukata wa JPM.
Kwa kuanzia simu hizi zitapatikana katika maduka ya mtandaoni yaliyo nchini marekani lakini kama kutakuwa na uhitaji mkubwa ni wazi kwamba Apple wataongeza upatikanaji wa simu hizi.
Kwa wanaonunua simu hizi huokoa hadi kiasi cha Dola za kimarekani 100 kwa kupata bei punguzo, simu nyingi za iPhone zipo katika mpango huu lakini pia matoleo ya hivi karibuni kama vile iPhone 6 na iPhone 6s ni moja ya matoleo ambayo yanauzwa katika mpango huu.
Endelea kutembelea mtandao wa Teknokona kwa taarifa mbalimbali za teknolojia katika lugha yako ya kiswahili.