Siku chache kabla ya kuanza kuuzwa kwa iPhone X, imeripotiwa kuwa kampuni ya Apple imemfukuza mmoja wa wahandisi wake baada ya binti wa mhandisi huyo kuweka video ya simu ya iPhone X kabla ya uzinduzi wake rasmi.
Binti wa mhandisi huyo anayefahamika kwa jina la Brooke Amelia Peterson alisema baba yake amefukuzwa kazi kwa kosa la yeye kuweka video katika ukurasa wake wa Yuotube ambayo video hiyo ilisambaa sana katika tovuti na blogu za habari za teknolojia.
Alisema baba yake alifukuzwa kazi kwa kuvunja sera ya kampuni ya Apple ambayo inazuia kupiga picha eneo la Kampasi ya Apple na iPhone X ambayo ilikuwa bado haijazinduliwa rasmi.
Fahamu kwamba wafanyakazi wenye nafasi za juu katika kampuni ya Apple huruhusiwa kuanza kutumia simu au vifaa vipya vinavyotengenezwa ambavyo bado havijazinduliwa.
Kisa kinaeleza kwamba binti huyo alienda kumtembelea baba yake akiwa pamoja na mama yake kupata chakula cha pamoja katika mgahawa maalumu kwa ajili ya wafanyakazi wa Apple. Wakiwa katika mgahawa huo binti alichukua simu ya baba yake na kuanza kuchukua picha za video na kisha kuionesha simu hiyo jinsi ilivyo na inavyofanya kazi kwa kuiweka katika akaunti yake ya Youtube.
Baada ya video hiyo kusambaa sana Apple walimwambia aitoe katika akaunti yake na alifanya hivyo. Kwa mujibu wa binti huyo anasema baba yake alifukuzwa kazi ambayo alikuwa amedumu kwa miaka minne.