Jumatano ilikuwa ni siku muhimu kwa Tanzania kiuchumi baada ya bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017 kusomwa bungeni, Teknokona kama waadau wengine tulikuwa makini tukifuatilia hotuba ya waziri wa fedha Mhe. Dkt. Philip I Mpango.
Makala hii inajadili baadhi ya mambo ambayo kwa namna moja ama nyingine yanaigusa sekta ya teknolojia ambayo yalijadiliwa katika bajeti hiyo.
Kuongeza uzalishaji Viwandani
kama kauli mbiu ya bajeti hii ya mwaka 2016/2017 inavyosema kuongeza uzalishaji viwandani ili kupanua fursa za ajira serikali imetenga kiasi cha bilioni 50.9 kugharamia tafiti za viwanda kupitia taasisi mbalimbali ikiwamo COSTECH pia kiasi hicho cha pesa kinategemea kuboresha miundombinu ya viwanda vidogo kupitia SIDO ili kuhakikisha tekolojia rahisi inapatikana kwa matumizi ya viwandani.
Miundombinu na Usafirishaji
Pia waziri alilijulisha bunge katika bajeti hii serikali imetenga kiasi cha fedha cha kutosha kujenga reli ya kati kwa kiwango cha standard gauge, kununua ndege tatu za Abiria, kununua meli mpya ziwa Viktoria, ukarabati wa meli ziwa Viktoria na Tanganyika. Pia kipo kasi cha kutosha kwaajiri ya kununua mabehewa na vichwa vya treni.
Nishati
Serikali katika bajeti hii pia imetenga fedha kwaajiri ya kukamilisha miradi ya umeme inayoendelea na pia kwaajiri ya kuongeza mitambo yenye uwezo wa MW185 katika mradi wa kinyerezi I na II.
Mazingira
Katika hatua za kulinda mazingira serikali imepiga marufuku utengenezwaji, utumiaji na unuzi wa mifuko ya plastiki ambayo ipo chini ya unene wa micron 50.
Huduma za pesa katika simu
Kutoza ushuru wa bidhaa wa asilimia 10 kwenye ada zinazotozwa na watoa huduma wa simu katika kutuma na kupokea fedha badala ya ushuru huo kutozwa tu kwenye kutuma fedha pekee. Waziri anasema kwamba utaratibu wa zamani baadhi ya kampuni zinazotoa huduma zimetumia mwanya kwa kuhamishia sehemu kubwa ya ada hizo kwenye kupokea fedha na hivyo kuwa nje ya wigo wa kodi.
Matumizi ya mashine za kielektroniki katika huduma za biashara
Aidha waziri wa Fedha alisisitiza kwamba serikali itasimamia kikamilifu matumizi ya vifaa na mifumo ya kielektroniki katika ukusanyaji wa mapato ili kuongeza ufanisi na kudhibiti upotevu wa mapato; na kuwasihi wananchi wote kudai risiti zinazotolewa na mashine za EFD ili serikali iweze kukusanya kodi zote stahiki.