Baada ya kupigwa vita huduma yake ya Freebasic ambayo kimsingi inalenga kuwapatia watumiaji wa mtandao huduma za intaneti bure hasa katika kutembelea mitandao michache muhimu, Facebook wameleta huduma nyingine ya Express WiFi ambayo inalengo la kufikisha intaneti katika maeneo ya vijijini.
Express Wifi ni huduma kutoka Facebook ambayo inaweza kumpatia intaneti mtumiaji kupitia hotspots za umma, tayari huduma hii imekwisha fanyiwa majaribio huko India na kufaulu kipindi cha majaribio.
Huduma hii inatofauti gani na huduma ya Freebasics!?
Tayari huduma ya Freebasics iligonga ukuta huko India baada mamlaka ya husika kuifungia kufuatia malalamiko ya kukiuka sheria za ushindani wa kibiashara. Hata hivyo safari hii huduma hii haitakuwa bure kwani mtumiaji atahitaji kulipia kadiri anavyotumia.
Huduma hii itafanyaje kazi lakini?
Facebook wanawatumia watoa huduma za intaneti (ISP), mitandao ya simu na pia makampuni binafsi katika miji husika ambao wao ndiyo watatoa huduma hiyo ya intanet kupitia hotspots za umma kwa kutumia program maalumu ambayo itatolewa na Facebook.
Hii inamaana gani kwa nchi kama Tanzania?
Kutokana na matokeo ya hudma hii huko India pengine huduma hii itasambaa katika mataifa mengine ambayo yanaendelea kama vile Tanzania na pengine yatabadilisha mfumo mzima wa upatikanaji wa huduma za intaneti.