Facebook inajulikana kwa kuwa mtandao wa kijamii ambao maudhui yake ni kwa watu mbalimbali kufahamiana, kukutanisha watu walioopotezana kwa muda mrefu pamoja na mambo mengine lakini imeonekana dhahiri kuwa fursa ipo kwenye ulimwengu wa mahaba.
Facebook inataka kufungua ukurasa mpya kwa kuja na programu tumishi ambayo maudhui yake ni kwa ajili ya watu wanaotafuta wapenzi. Katika mkutano wa Facebook F8 mwezi Mei 2018, Bw. Zuckerberg aliweka wazi kuwa Facebook ilikuwa unatengeneza programu tumishi ambayo itakuwa inahusu “Ulimwengu wa mahaba”.
Suala hilo ambalo liliibuliwa na mchunguzi wa suala ya programu tumishi, Bi. Jane Manchun Wong ambae mara nyingi amekuwa akiibua vitu vipya ambayo Facebook itavileta kwa mara nyingine ameweza kuwweka ushahidi wa kuwa Facebook wanaifanyia majaribio programu tumishi mpya inalenga watu kuweza kutafuta wapenzi.
Kwa mujibu wa Bi. Jane hivi sasa programu hiyo inajaribiwa na wafanyakazi wa Facebook nchini Marekani lakini kwa kuweka taarifa zao za uongo kama hatua ya majaribio ili kuona ufanisi wa programu hiyo.
Kwenye programu hiyo tumishi imeonekana kuwa mtumiaji anaweza kupangilia nani na nani wanaweza kuona/kutoona sifa zake, kuweka wazi au la jinsia ya mhusika na hata kusema ni mwanaume/mwanamke wa aina mlengwa anamhitaji.
Kwanini iwe programu tumishi inayohusu ulimwengu wa mahaba?
Wamiliki wa tovuti/programu tumishi zinazosaidia kutafuta wapenzi zimeonekana kujipatia kipato kutokana na kwamba inafikia kipindi kama unataka kufanya mawasilaiano na mhusika basi itakubidi ulipie kiasi fulani cha pesa, sasa hiyo si itakuwa fursa ya Facebook kujiongezea kipato?
Lakini pia kwa mujibu wa uchunguzi wa mwaka 2013 ulibaini kuwa 77% ya watu wanaona tovuti/programu tumishi zinazohusu kutafuta wapenzi ni muhimu sana kwao kuwa nazo kwenye simu.
Vilevile, 15% ya Wamarekani walikiri kuwa wameshawahi kujiunga kwenye tovuti ya kutafuta wapenzi/walishawahi kutumia programu tumishi za namna hiyo.
Pengine suala hili likaishia katika hatua za majaribio tena kwa watu wachache kwani Facebook inajulikana kwa kujaribisha vitu halafu mwisho wa siku vinaishia hatua hiyo hiyo bila kupelekwa kwa walengwa.
Vyanzo: Engadget, The Verge na Psychology Today