Mtandao maarufu wa Kijamii wa Facebook umetangaza kuongeza faragha kwa watumiaji wake kwa kuweka sehemu ya kufuta historia ya walichokitafuta (search) katika mtandao huo wa kijamii.
Mtandao huo umefikia uamuzi huo baada ya hivi karibuni kukumbwa na kashfa ya kutolinda faragha za watumiaje wake huku zaidi ya watu 50 millioni wakidaiwa kudukuliwa taarifa zao katika kipindi cha uchaguzi wa Marekani.
Inaelezwa katika sakata hilo mamilioni ya taarifa za watumiaji zilichukuliwa bila ridhaa na kampuni ya Cambridge Analytical kwa matumizi ya wanasiasa. Mkurugenzi Mtendaji na mwanzilishi mwenza wa Facebook, Bw. Mark Zuckerberg aliwahakikisha watumiaji wa mtandao huo kwamba suala kama hilo halitajitokeza tena kwa kuweka ulinzi zaidi.
Kupitia mkutano wa mwaka wa kampuni ya Facebook Mark, Zuckerberg alisema kwamba kilichotokea kwa Cambridge Analytical ni uvunjifu wa uaminifu wa hali ya juu, wakichukua data za watu na kuziuza hivyo watahakikisha suala hilo halitokei tena kwa kuweka vizuizi kwa data ambapo mtu atakua anaombwa kwa ridhaa yake, na kuondoa programu zote mbaya zilizopo kwenye mtandao huo wa kijamii.
Uimarishwaji huo wa ulinzi kwa Facebook sasa utamruhusu mtumiaji wake kuweza kufuta historia ya kile alichokitafuta kupitia mtandao huo.