Hivi karibuni Facebook imechukua hatua nyingine ya kupambana na kile kinachoitwa habari za uwongo.
Kwa siku za usoni, kampuni ya Facebook itazuia huduma ya kujitangaza kwa muda usiojulikana kwa kampuni na kurasa zote zitakazotumia kurasa zake kusambaza habari za uwongo.
Facebook kuzifungia kurasa zote kujitangaza ikiwa zitasambaza habari za uwongo: Hii ina maanisha kurasa hizo zitashindwa kutumia huduma ya kibiashara ya kimatangazo kwenye mtandao huu maarufu.
“Habari za uwongo zinaharibu imani ya watu walioko kwenye Facebook” Mkurugenzi wa bidhaa wa Facebook Rob Leathern aliyasema hayo. “Hatutaki kurasa zinazosambaza habari za uwongo kuongeza wafuasi na kusambaa zaidi kwenye Facebook” Kwa hiyo tumeamua kufanya hivi ili jamii ifahamu.
Facebook ilikataa kubainisha ni mara ngapi hasa ukurasa husika ukisambaza habari hizo utafungiwa. Pia hawakubainisha kufungiwa huko kutadumu kwa muda gani.
Leathern aliendelea kusema kuwa “Hatutaki kulibainisha hili; kwani hatutaki watu wacheze na mfumo wetu”
Tangazo hili la hivi karibuni ni moja kati ya jitihada za Facebook za kupambana na tatizo la habari za uwongo lililoibuka miaka ya hivi karibuni. Mnamo mwezi Mei Facebook iliongeza vipengele vinavyowawezesha watumiaji wake kubainisha maudhui wasiyopenda kuyaona pamoja na yale yenye ubora mdogo.
Mapema mwezi huu Facebook imeanza kutumia teknolojia maalumu ya kukagua maudhui yanayohisiwa kuwa mabaya ili kutuma onyo kwa wahusika.
Tangazo hili la hivi karibuni linakuja baada ya uchaguzi wa mwaka uliyopita wa raisi nchini Marekani ambapo Facebook ilikosolewa vikali kwa kusambaza habari za uwongo. Jambo hili liliibuka tena mnamo mwezi Mei pale ambapo wapigakura wa Ufaransa waliilaumu Facebook kwa kusambaza habari za uongo kuhusu uchaguzi wa rais nchini humo.
Huko Ujerumani nako bunge lilipitisha sheria ya kutaka mitandao ya kijamii kuondoa hotuba za chuki ndani ya saa 24 zitakazowekwa kwenye mitandao husika.