Facebook na kampuni ya kutoa ushauri wa kisiasa ya Cambridge Analytica zimeshtakiwa nchini Marekani kwa kutoa habari za siri za zaidi ya watu 50 milioni wanaotumia huduma za mtandao huo wa kijamii bila idhini yao.
Kesi hiyo iliyowasilishwa Jumanne jioni na Lauren Price, mkazi wa Maryland, ni ya kwanza dhidi ya Facebook kutokana na kutomakinika kwake kulinda data za wateja wake. Pia ni kesi ya kwanza dhidi ya Cambridge Analytica kwa kutumia data hizo bila idhini kwa ajili ya kusaidia kampeni za rais Donald Trump kuelekea uchaguzi wa Novemba 2016.
Kila mtumiaji mtandao wa Facebook ni mhusika katika kesi hii kwani data zao zilitwaliwa bila idhini yao. Kwa hivyo, haki yao ya usiri imeingiliwa-John Yanchunis, wakili wa Bi. Price.
Kesi hiyo iliwasilishwa saa kadhaa baada ya Facebook kuelekezewa lawama katika kesi nyingine iliyowasilishwa na mwenye-hisa mmoja aliyedai bei ya hisa zake zilishuka baada ya sakata hilo kufichuliwa. Kesi hiyo ya pili iliwasilishwa katika mahakama ya San Francisco.
Facebook ilikiuka sera yake kuhusu usiri kwa kutoa maelezo/data za wateja wake bila idhini yao. Mbali na hapo bei ya hisa za Facebook ilipungua kwa takribani dola 50 bilioni (Tsh 5 bilioni) kwa kipindi cha siku mbili pekee.
Wakili wa mlalamikaji anasema Bi. Price alikuwa akipata jumbe za kisiasa katika ukurasa wake wa Facebook wakati wa kipindi cha kampeni. Bi Price hakuwa amewahi kuona jumbe kama hizo wakati mwingine. Vilevile, hakuelewa kilichokuwa kikiendelea wakati huo lakini sasa ameng’amua kuwa jumbe hizo zililenga kumshawishi kupigia kura chama fulani.