Microsoft wanafanyia kazi sasisho (update) jipya la Windows 10 litakaloleta uwezo wa kubofya na kuifanya Windows 10 ikae kwa ajili ya kuchezewa magemu – yaani kuwa na ‘Game Mode’.
Tayari Windows 10 imeonekana kupendwa kama Windows 7 kwa watumiaji kompyuta zao kwa ajili ya uchezaji magemu na inaonekana Microsoft wameona umuhimu kuifanya programu endeshaji hii kuzidi kuwa rafiki kwa watu hao.
Kutakuwa na kisehemu cha kubofya kwenye Windows 10 na mara moja kompyuta itaingia kwenye ‘Game Mode’, ikiwa kwenye Game Mode programu endeshaji ya Windows 10 itajizatiti kuhakikisha magemu yanachezeka kwenye ubora mzuri zaidi ukilinganisha na kama gemu hilo hilo likichezeshwa bila uwepo wa Game Mode.
Kwa sasa uwezo huu upo katika majaribio kwa wale wanaotumia toleo la Windows 10 la majaribio (Windows Insider Preview) na inategemewa utaletwa kwa watumiaji wa Windows 10 kupitia masasisho (updates) kipindi chochote kuanzia sasa.