Google wakamilisha kuwanunua wahandisi 2,000 wa HTC ili kuzidi kujikita katika utengenezaji wa simu zake za familia ya Pixel.
Google wamejaribu mara kadhaa kuingia kwenye biashara ya utengenezaji simu hii ikiwa ni pamoja na kuja na simu za Nexus ambazo walikuwa wakizifanyia ubunifu na kisha kuacha makampuni mengine kama vile HTC, LG, Motorola na mengine kuzitengeneza.
Kwa sasa Google wamekuwa wakileta simu za Google Pixels, katika utengenezaji wa simu hizi Google wamekuwa wakichukua nafasi kubwa katika ubunifu na utengenezaji wa programu endeshaji – toleo la Android spesheli, ili kuhakikisha simu inakuwa katika ubora wa hali ya juu.
Simu za Google Pixels zimesifika na ndio zimekuwa simu za kwanza kuwa na sifa ya kuweza kushindana na simu zingine za juu kama vile iPhone na simu za familia ya Samsung Galaxy S na Galaxy Note.
Kutokana na mafanikio ambayo wameyapata kupitia simu za Google Pixels, Google kwa sasa wanataka kuzidi kujikita katika utengenezaji wa simu hizo kwa kuwa na timu ya ndani badala ya kutumia ushirikiano na makampuni mengine kama vile HTC, LG na wengine – hali ilivyokuwa zamani.
Google wameamua kununua wahandisi wa HTC (Design engineers) wote waliokuwa wakihusisha na kazi za ubunifu mkubwa wa vipuli vya utengenezaji wa simu za Google Pixels ndani ya kampuni ya HTC. Hii ina maanisha kwa sasa Google watakuwa na uwezo mkubwa wa kubuni vitu vyote – programu endeshaji spesheli na vipuli vya simu husika.
Google wameilipa HTC dola bilioni 1.1 kwa ajili ya kuwachukua wafanyakazi 2,000 kutoka HTC. Bado HTC wamesema wao pia wataendelea na utengenezaji wa simu za jina lake. Wafanyakazi hao 2,000 walikuwa ni nusu ya idadi ya wafanyakazi wao wote wa kitengo cha utafiti na ubunifu – katika teknolojia za simu.
Kwa sasa inaonekana kuna faida kubwa kufanya hivyo ili kuhakikisha programu endeshaji inafanya kazi katika ubora wa hali ya juu. Kwa miaka mingi Google wamekuwa wakiamini makampuni ya simu kama vile Samsung, HTC, na wengine bado hawatengenezi simu zenye ubora wa kuifanya programu endeshaji ya Android iwe kwenye utendaji bora zaidi na hivyo ata kuweza kushindana na simu za iPhone sokoni.
Faida ya kutumia simu za Google Pixels;
- Utapata masasisho (updates/upgrade) za matoleo ya Android kwa wakati na kwa miaka mingi zaidi.
- Google kama watengenezaji wa Android wanahakikisha simu inafanya kazi kwa ufanisi zaidi kwa kuwa wana simamia utengenezaji wa vitu vyote viwili muhimu – programu endeshaji na kifaa (simu) husika
Je hii ina maanisha Google watakuwa na kiwanda cha utengenezaji simu?
Hapana. Wengi bado wanaamini njia inayochukuliwa na Google itakuwa sawa na ile iliyochukuliwa na Apple. Hii ikimaanisha watakuwa wanafanya ubunifu wa vitu vyote muhimu vya kutumika kwenye simu zao – hii ikiwa ni pamoja na prosesa n.k, na kisha kuingia mikataba na kampuni kama Foxconn ambayo ndio itatengeneza vifaa hivyo na kisha Google au Foxconn kumalizia kwenye uundaji wa simu husika kwa kutumia vipuli hivyo.