Simu janja zenye kutumia mfumo endeshi wa Android ndio zinazotumika kwa wingi kulinganisha na simu janja zenye kutumia mifumo endeshi mingine na kuifanya Android kuwa moja ya programu endeshaji maarufu duniani.
Google ambayo ni moja kati ya kampuni nguli na kongwe katika masuala ya teknolojia imeweka bayana kuwa imekuwa ikiwafuatilia watumiaji wa simu za Android hata kama mtu akiwa hataki kufuatilia (kuzima kipengele cha location) jambo linaweza kuwa limewashangaza wengi kutokana na kuamini kuwa iwapo umezima kipengele cha location basi hakuna mtu atakayeweza kujua sehemu ulipo.
Je, Google ilianza lini kufuatilia simu za wateja wao?
Usiwe na shaka msomaji wetu, Google hawajaanza muda mrefu kufuatilia simu janja za wateja wao na wameweka wazi kuwa walianza kufuatilia simu za Android mwanzoni mwa mwaka 2017 kwa kufuatilia tarakimu zisizofanana (Cell ID) na kisha kutuma taarifa hizo kwenda Google hata kama simu janja imezimwa na sim card imetolewa 🙄 🙄 🙄 .
Katika ufuatiliaji huo wa Google iliomba Cell ID, tarakimu za kimawasiliano kwa utambulisho wa nchi na tarakimu zisizofanana za mtandao ambao mtu anatumia kwenye simu janja yake ambao uliwezesha kujua mpaka mtandao wa simu ambao mhusika anatumia.
Unaweza ukajiuliza je, kwanini Google imekuwa ikifuatilia simu za Android? Sababu waliyoisema ni kuwa na nia ya dhati ya kuboresha utendaji kazi wa simu husika na jinsi ambayo wameweka mipangilio yao ni kuchukua taarifa hizo, kufanya maboresho pamoja na kujifuta zenyewe baada ya muda mchache na kubwa zaidi ni kutotuma ombi la kuchukua tena taarifa hizo.
Mtindo wa kufuatilia wateja wake ni kitendo ambacho makampuni mengi tu yanakifanya ila ni kwa sababu tu hawajitokezi hadharani na kukiri hilo. Google imesema itaacha kitendo cha kufuatilia simu janja za Android mwisho wa mwezi Novemba 2017.
Vyanzo: The Guardian, The News Minute