Huwa jambo la kupendeza na kujivunia tunapozidi kuona apps nyingi za kiutofauti zinapotengenezwa na watanzania. App hii inayokuwezesha kufahamu matumizi ya pesa zako za ‘mobile money’ imetengenezwa na kampuni inayoenda na jina Nabure.
Miaka ya hivi karibuni tumeweza kuona ukuaji wa apps zinazotengenezwa nchini na huku walengwa katika utumiaji ikiwa ni watanzania mfano app ya mPaper na Hadithi. Kampuni ya Nabure ilianzishwa na kijana Ian Manyama – @iannashin na utengenezaji wa app hii ulihusisha vijana wengine watatu.
App ya Hakiki inakusaidia nini hasa?
App ya Hakiki inatumia ujumbe wa SMS unaopokea kutoka mtandao wako unaotumia kwa huduma za kibenki za simu kukutengenezea ripoti, kwa sasa inaweza kutengeneza ripoti za mpesa, Airtel money, na Tigo pesa.
Nje ya kutengeneza ripoti utaweza ata kupanga bajeti zako na app hiyo itakuwa inajaza taarifa za matumizi kulingana na ujumbe unaopokea kutoka mtandao wako wa simu.
Jinsi ilivyo
> Nilivyoipakua na kuifungua mara ya kwanza ilinipeleka kwenye ukurasa wa mipangilio ambapo unaweza weka mambo kadhaa sawa;
- Kuchagua lugha
- Kuweka ulinzi wa ‘password’ ili mtu mwingine asiweze ingia
- Pia utaweza chagua huduma ya pesa unayotumia – MPESA, Airtel Money au Tigo Pesa.
> Pia ripoti zinajumuhisha pia taarifa za mapato, hii iwe kama umeweka mwenyewe pesa au umetumiwa pesa.
Usalama?
Nabure wanasema app hiyo haitumi taarifa zozote kuhusu matumizi yako. Kinachofanywa na app hiyo ni kuchambua tuu ujumbe wa sms za malipo na mapokeo ya pesa na hivyo kutumia data hizo katika kukutengenezea ripoti. Hakuna taarifa inayotoka.
Mtazamo wangu
Baada ya kuijaribisha katika simu yangu yenye laini ya Airtel ambayo pia huwa inafanya mihamala ya Airtel Money kwa zaidi ya asilimia 90 imeenda sahihi kabisa.
Ripoti zilikuwa sahihi zikionesha mapato na matumizi ila kidogo kwenye mapato kulikuwa na makosa. Mfano; Kama mtu ukinunua umeme kupitia Airtel money basi huwa kuna ofa za muda wa maongezi huwa zinatolewa, mfano Tsh 1,000. App imechanganya na kuingiza mapato hayo ya vocha kwenye jumla ya salio la Airtel Money.
Kwa kiasi kikubwa hii app itakuwa msaada kwa wengi wanaofanya mihamala mingi kwa mwezi bila kufuatilia kwa umakini juu ya mihamala wanayoifanya. Kwa wingi wa huduma zinazoweza lipiwa kwa kutumia huduma za kibenki za simu watu wengi wamejikuta wakitumia huduma hizi kufanya malipo mbalimbali ya kila siku kwa kutumia huduma hizi.
Je kwa sasa unaweka rekodi ya mihamala yako unayofanya kwenye huduma za kibenki za simu?
[socialpoll id=”2380705″]
Unaweza pakua app ya Hakiki kupitia Google Playstore