Wakati LG, Samsung na Huawei wakitaka kuwa wa kwanza kuzindua simu janja yenye mkunjo hilo halitawezekana tena limewahiwa na kampuni isiyo na jina kubwa-Royole iliyo na makazi yake huko California, Marekani.
Kampuni hiyo imezindua simu yake mpya inayofahamika kama Royole FlexPai na ndio inatajwa kuwa simu janja ya kwanza kuwa ya mkunjo kuingia sokoni.
Simu hii, FlexPai ikikunjuliwa inakuwa na kioo cha urefu wa inchi 7.8 na kuwa na muonekano wa tabiti na ikikunjwa inakuwa na ukubwa kioo cha inchi 4 sawa na simu janja za kawaida. Teknolojia ya kwenye kioo ni AMOLED.
Mfumo endeshi wa simu hii utakuwa wa Android 9 Pie lakini upo mfumo endeshi mwingine wa kampuni hiyo unaofahamika kama WaterOS 1.0 utakaokuwa juu ya mfumo wa Android.
Kwa mujibu wa Royole simu hiyo inaweza kukunjwa na kukunjuliwa zaidi ya mara 200,000 bila ya kuharibika. Mfano mtumiaji awe na kawaida ya kukunja na kukunjua mara 100 kwa siku, itamchukua miaka 5 kuifikia idadi ya mikunjo 200,000.
Inaelezwa kwamba FlexPai itakuwa na kipuri mama-Qualcomm Snapdragon 8150 ambayo itakuwa na kasi zaidi kuliko simu zilizotolewa mwaka na 2018 na hata za mwaka 2019 lakinikampuni husika haijathibitisha kama ndio itakayotumika kwenye FlexPai au la!.
Kutakuwa na matoleo matatu yaliyo tofauti katika RAM na diski uhifadhi ambapo moja itakuwa na RAM 6GB/memori ya ndani-128GB, nyingine RAM 8GB/memori ya ndani-256GB na RAM 8GB/memori ya ndani-512GB.
Aidha, kwa upande wa kamera ya nyuma itakuwa na 16MP pamoja 20MP na kwa upande wa kamera ya mbele itakuwa kamera hiyo hiyo pale itakapokunjwa na kuwa na muonekano wa simu janja ya kawaida.