Mmiliki wa mtandao wa Facebook Mark Zuckerberg ametangaza malengo yake binafsi katika mwaka 2018 kupitia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Facebook.
Kwa miaka minane mfululizo Mark Zuckerberg amekuwa akiweka lengo moja ambalo anakuwa analitimiza kikamilifu katika mwaka husika.
Lengo alilotangaza mwaka huu (2018) ni kuahidi kurekebisha makosa yaliyotokea mwaka uliopita ya kushindwa kuzuia taarifa za uongo (Fake News) zilizokuwa zikisambazwa kupitia mtandao wa Facebook.
Kupitia ukurasa wake wa Facebook ameandika kuwa ataongeza juhudi katika kulinda kanuni na kuzuia matumizi mabaya ya mtandao, katika masuala muhimu aliyoyataja kama kuilinda jamii dhidi ya unyanyasaji na chuki.
Pia kudhibiti taarifa dhidi ya mataifa yanayoingia kati masuala ya mataifa mengine, na kuhakikisha kwamba muda unaotumiwa kwenye Facebook unatumiwa vizuri na kwa maslahi mazuri.
Kuenezwa taarifa za uongo kupitia Facebook ni jambo lililoshamiri sana kiasi cha kufanya matumizi ya mitandao kuonekana kama sehemu ya kubadilishana uongo na habari za kipuuzi na hivyo kupoteza maana nzima ya mitandao ya kijamii.
Utaratibu wa kuweka lengo moja kwa kila mwaka kwa Mark Zuckerberg ulianza mwaka 2009 alipoweka azma ya Kuvaa tai kila siku, na mwaka 2010 aliweka lengo la kujifunza lugha ya kichina ya Mandarin na mwaka 2010 kula nyama ambayo amechinja mwenyewe.
Mwaka 2013 aliweka lengo la kukutana na mtu mmoja kila siku nje ya Facebook. Mwaka 2015, kusoma kitabu kila wiki. Mwaka 2016, kutengeneza roboti wa kuendesha shughuli za nyumbani kwake na mwaka 2017 kutembelea majimbo yote nchini Marekani na kukimbia maili 365.