Katika kipindi cha wiki moja taarifa juu ya huduma ya iCloud kuhamia China ilisambaa sana. Je ni watumiaji wote wa iPhone, iPad na Mac wataathirika na hili? Fahamu zaidi.
Kwa ufupi kuna makampuni mengi makubwa yamejaribu na kushindwa kufanya biashara nchini China. Mara nyingi makampuni mengi yameshindwa kukubaliana na sheria kali zinazohusu suala la data za watumiaji wa huduma mbalimbali za kimtandao zinazosimamia wananchi wa China.
Serikali ya nchini humo inapenda kuwa na mfumo unaowezesha vyombo vyake vya sheria urahisi wa kupata na kuzisoma data za mtu yeyote aliye nchini humo.
Tayari Google walishashindwa kufuata sheria hiyo na hivyo kujikuta ikiwalazimu kufunga biashara zake nchini humo. Huduma mbalimbali za Google hazipatikani nchini China.
Pia ata Facebook alishindwa kuzikubali sheria hizo na hadi sasa huduma ya Facebook haipatikani nchini humo. Ingawa tayari mkurugenzi wake Bwana Zack anafanya kila awezalo kujenga mahusiano ya karibu na uongozi wa nchi hiyo kuona kama watapata baraka bila kuathiri misingi yake. Lakini hadi sasa hajafanikiwa.
Kwa Apple walishajikuta kwenye wakati mgumu kisheria, huduma ya iCloud inayokuja katika vifaa vyake mbalimbali hii ikiwa ni pamoja na iPhone, iPad na laptop/kompyuta zake za Mac, imekuwa ikihifadhi data nje ya nchi hiyo. Wakajikuta kwenye kuchagua mawili; wauze simu za iPhone nchini humo bila huduma ya iCloud, au wakabali huduma ya iCloud kwa watumiaji wa nchini China kuhifadhi data zake nchini humo humo.
Ili kutolikosa soko la simu kubwa duniani la China, Apple wamejikuta wakikubaliana na sheria za nchini humo. Na sasa watatumia kampuni ya China yenye mahusiano ya karibu na serikali ya nchini humo katika uhifadhi wa data za watumiaji wa huduma ya iCloud wa nchini humo.