Kama ilivyotabiriwa, nchi ya India sasa imeipita Marekani na kuwa soko la pili kwa ukubwa wa uuzwaji wa simu janja za Android ulimwenguni.
Kwa mujibu wa kampuni huru ya uchambuzi ya Canalys kwamba soko la India limekuwa kubwa zaidi la pili duniani baada ya soko la Uchina. Taarifa hiyo imeangalia makampuni matano makubwa ya uzalishaji simu janja ambapo kampuni ya Samsung na Xiaomi wameendelea kuwa karibu kwa mauzo yanayofikia takribani nusu ya simu zote zinazouzwa nchini India.
Mauzo ya Xiaomi kutoka robo ya tatu ya mwaka 2016 mpaka robo tatu ya mwaka 2017 yamepanda kwa asilimia 290. Ukuaji wa Xiaomi umeonekana kutishia soko la Samsung nchini India. India ambayo uchumi wake unakua kwa kasi na licha ya changamoto ya kisiasa na kijamii mahitaji ya simu yameongezeka kwa kiasi kikubwa tofauti na miaka michache iliyopita.
Wazalishaji wengi wa simu janja wamekuwa na lengo la kufanya India kuwa sehemu ya uwekezaji na kituo kikubwa cha teknolojia ya kimataifa. Hata hivyo, simu za Vivo, Oppo na Lenovo zimekuwa zikifanya vizuri kwa mauzo nchini India.
Ukuaji wa Xiaomi kununuliwa na wengi nchini India kumechangia na unafuu wa bei zake kulinganisha na Samsung, Oppo, Vivo na Lenovo.
Ongezeko la uuzaji wa simu janja kwa soko la India limeongezeka kwa asilimia 23 kulinganisha na mwaka uliopita. Kampuni hizo tano ndio zilizoangaziwa kwa kuwa zimekuwa zikichangia mauzo ya simu kwa asilimia 75 ya zote zinazouzwa nchini India.
Kuna aina ya simu tofauti zinazokadiriwa kufika 100 zinazouzwa nchini India hivyo kufanya kuwa moja ya soko gumu zaidi duniani. India ni nchi yenye watu wengi zaidi duniani nyuma ya nchi ya China, lakini changamoto kubwa ni pato kwa mwanachi wa kawaida kumudu kununua simu janja.