Mahakama moja nchini Italia imetoa hukumu kwa mfanyakazi wa kampuni ya Telecom Italia kulipwa fidia kwa kupatwa na uvimbe katika ubongo uliosababishwa na matumizi ya muda mrefu ya simu ya mkononi.
Mahakama hiyo iliyopo kaskazini mwa mji wa Ivrea ilitoa hukumu hiyo Aprili 11, 2017 kwa Roberto Romeo mwenye umri wa miaka 57 ambaye bado mfanyakazi wa kampuni aliyoishitaki.
Kesi hii inakuwa ya kwanza duniani kutolewa hukumu ya namna hiyo kwa mahakama kutambua matumizi makubwa ya simu ya mkononi kunasababisha uvimbe katika ubongo.
Romeo alifungua kesi ya kulalamika kwamba alilazimika kutumia muda mrefu kuzungumza na simu ya mkononi kulikosababishwa na kazi alizopewa na kusimamia.
Alithibitisha kwamba majukumu ya kazi yake yalimlazimu atumie simu yake kwa saa tatu hadi nne kila siku za kazi kwa muda wa miaka 15 kuwapigia simu wafanyakazi wenzake kwa ajili yakuandaa mipango ya kazi kwa siku husika.
Alisema, “Sikuwa na chaguo bali kutumia simu yangu kuzungumza na wafanyakazi wenzangu na kuandaa kazi. Kwa miaka 15 nilikuwa nalazimika kuwapigia wote, kuanzia nyumbani, katika gari mpaka ofisi.”
Aliongeza kusema, “Nilianza kuhisia sikio langu la kulia kuwa limefunga (halisikii) kabisa muda wote na mwaka 2010 ubongo wangu uligundulika kuwa na uvimbe. Furaha yangu ilitoweka kwa kuwa sikuweza tena kusikia kwa sikio hilo.”
Kwa mujibu wa mtaalamu wa matibabu inakadiriwa asilimia 23 ya madhara ya afya yake yamesababishwa na matumizi ya simu aliyokuwa akiyafanya akiwa kazini kwake kwa muda wa miaka 15.
Hakimu wa mahakama hiyo alitoa hukumu kwa Romeo kulipwa zaidi ya takribani milioni 1 ya kitanzania kila mwezi kama fidia kupitia mfuko wa Taasisi ya Bima ya Taifa Ajali Kazini ya italia (INAIL) ya kupata ajali mahala pa kazi.
Romeo alitarajia kulipwa mamilioni ya pesa kama fidia ya mwaka huu. Tafiti za kisayansi zinasema kuna hatari ya kiafya katika matumizi ya simu za mkononi yanayopita kiasi kwa mtumiaji. Lakini kuna wengi wanaona bado utafiti mkubwa juu ya madhara ya utumiaji simu za mkononi kwa mazungumzo ya muda mrefu.
Hata hivyo watafiti hao wanasema ni mapema kulithibitisha hilo kulingana na teknolojia mpya na za kisasa za uundaji simu zinazojaribu kupunguza mathara ya utumiaji simu za mkononi.