Kupitia makubaliano na makampuni kadhaa ya mawasiliano na kampuni ya ZTE, mitandao ya mawasiliano ya nchini Japani inaweza ikawa ya kwanza kwa huduma nzuri ya intaneti ya 5G.
Makampuni mbalimbali ya kimawasiliano ya nchini China kama vile ZTE na Huawei wamejikuta katika wakati mgumu kisheria na kibiashara nchini Marekani, serikali ya nchini humo ikidai utumiaji wa bidhaa na teknolojia za makampuni hayo si salama kwani kuna uwezekano mkubwa serikali ya China ikawa na uwezo wa kuona/kudukua data za mtumiaji.
Mitambo ya teknolojia ya 5G inayotengenezwa na ZTE inaonekana kuwa ya bei nafuu zaidi kwa makampuni ya mawasiliano ukilinganisha na vyanzo vingine.
Mtandao wa Nikkei Asian Review umesema tayari ZTE ipo katika mazungumzo na makampuni kadhaa ya nchini Japani ili kufanikisha uwekaji wa mitambo ya huduma ya intaneti kwenye kasi ya 5G ili kufanikisha uwepo wa teknolojia hiyo kabla ya mashindano ya Olympics ya jijini Tokyo ya mwaka 2020.
Ripoti zinaonesha gharama ya mitambo ya 5G kutoka ZTE ni nafuu, takribani 1/5 ya gharama za mitambo hiyo hiyo kutoka kwa watengenezaji kutoka nchi za barani Ulaya na Japani.
Serikali ya Marekani inawashauri wananchi na mashirika ya nchini humo kutonunua simu zinazotengenezwa na ZTE na Huawei, na kwa wakati huo huo wanayabana makampuni ya simu kutotegemea kabisa bidhaa/teknolojia kutoka makampuni hayo.