Twitter imewashauri watumiaji wake milioni 336 kubadili nywila (nenosiri) zao baada ya kugundua tatizo katika mfumo wa utunzaji wake lililotokea katika mtandao huo kusababisha nywila zao kuweza kusomeka.
Tatizo hilo lilisababisha nywila za watumiaji wa Twitter zionekane katika maandishi ya wazi hivyo kuweza kudukuliwa kwa akaunti ya mtu. Hata hivyo, mtandao huo wa kijamii (Twitter) umesema kuwa uchunguzi umeonyesha kuwa hakuna nywila zilizoibwa. Kwa tahadhari Twitter imewataka watumiaji wake kubadilisha nenosiri kwenye Twitter.
Twitter haijasema ni nywila ngapi ziliathiriwa na tatizo hilo lakini chanzo kimoja kiliambia shirika la habari la Reuters kwamba idadi ya akaunti zilizoathiriwa ni kubwa na kwamba nywila zilikuwa zikionekana kwa miezi kadhaa; yaani kutokuwa katika mfumo wa nyota (*).
Unaweza kutumia njia mbili za kuifanya akaunti yako kuwa salama au kutumia programu kama vile LastPass au 1Password kuzuia kabisa akaunti yako kuwa katika hatari ya kudukuliwa hata kama tatizo lilitokea kwa Twitter katika mfumo wa utunzaji nenosiri za watu likijirudia/kutokea kwa wengine.