Karibuni watumiaji wa mitandao ya kijamii nchini Uganda wanaoingia kupitia programu tumishi za VPN ili kuepuka kulipa kodi kwenye huduma za Over-the-Top (OTT) hawatakuwa na uwezo huo baada ya serikali ya Uganda kuzitaka kampuni za mawasiliano kuzuia programu hizo.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa tume ya mawasiliano ya Uganda, Bw. Gofrey Mutabazi amezitaka kampuni za simu kuanza kuzuia polepole programu tumishi za VPN ili wale wanaojaribu kukwepa kodi wasiweze kufungua mitandao ya kijamii inayotakiwa kulipiwa kodi kabla ya kuitumia.
Pamoja na mpango wa kuzuia matumizi ya VPN, Mutabazi amesema kuwa programu za VPN ni nyingi hivyo itakuwa ngumu kuzuia zote na watalazimika kuzifunga baadhi.
Kodi kwa mitandao ya kijamii imeanza kutumika nchini Uganda kwenye mwaka mpya wa fedha 2018/2019 (julai Mosi). Ambapo mwananchi anatakiwa kulipa shilingi za Uganda 200 kwa siku au 1,400 kwa wiki/6,060 kwa mwezi.
Zoezi hilo limeleta usumbufu kwa wananchi wengi nchini Uganda kiasi cha kuwafanya wengine kuanza kutumia programu tumishi za VPN ili kuperuzi mitandao ya kijamii bila ya kulipa kodi.
Moja ya kazi za VPN ni kumuonesha muhusika kwenye eneo ambalo sio halisi. Mfano mtumiaji yupo Uganda lakini kwa kutumia programu ya VPN anaweza kuonekana yupo Tanzania/Kenya au nchi yoyote atakayoamua aonekane.
Kwa kufanya hivyo ataweza kufungua mitandao ya kijamii iliyofungiwa Uganda kwa kuwa VPN inamuonesha kama mkazi asiyeishi Uganda. Kwa muda wa siku tatu watumiaji wa Intaneti nchini Uganda wamepakuwa programu za VPN zaidi ya mara milioni 1.5.