Fikiria kiwanja cha ndege kilichokuwa na safari nyingi sana kila muda ndege zinapaa na kutua – alafu sehemu ya kuongozea ndege na kutoa msaada wa kutua na kuondoka uwanjani hapo KUTOKUWA na mtu yeyote kabisa katika eneo hilo.
Basi ndio teknolojia inayokuja kwenye kiwanja cha ndege cha kimataifa cha London cha nchini Uingereza.
Kiwanja cha ndege hicho kinakuwa moja ya viwanja vichache duniani kote kuanza kutumia teknolojia kubwa ya kidigitali kuhakikisha huduma inaboreshwa kwa kutumia teknolojia za kisasa hasa hasa kwenye masuala ya hali ya hewa na kamera za kisasa ili kumsaidia muongozaji ndege katika kiwanja cha ndege kuweza kujionea mengi zaidi na kwa urahisi zaidi.
Nini kipya?
Eneo la mnara wa kuongozea ndege hakutakuwa na watu ndani yake bali kutakuwa na kamera 14 zinazochukua picha (video) za moja kwa moja katika ubora wa HD. Pia kutakuwa na sensa mbalimbali za kuweza kugundua mabadiliko mbalimbali ya vitu eneo la uwanja. Kamera hizo zitaweza kuchukua picha za moja kwa moja za HD katika eneo la uwanja wa ndege.
- Video hizo za moja kwa moja, yaani mubashara zitakuwa zimeunganisha moja kwa moja kupitia nyaya za intaneti ya kisasa na haraka (fiber) na kutuma taarifa hizo moja kwa moja kwenye kijiji kingine kilicho umbali wa takribani kilometa 110 kutoka kiwanja hicho cha ndege.
- Katika ofisi ya kijiji hicho kutakuwa na vioo/display kubwa za kuonesha taarifa zote zinazopokelewa muda huo hii ikiwa ni pamoja na hali ya hewa na muonekano mzima wa eneo la kiwanja cha ndege.
Muongozaji ndege ataweza kuona mambo mengi kwa haraka na urahisi zaidi ukilinganisha na kama angekuwa kwenye chumba cha mnara wa kuongozea ndege katika kiwanja cha ndege.
Je ni salama dhidi ya udukuzi?
Kwa kiasi kikubwa itakuwa hatari sana kama mawasiliano ya kutoka kwenye kamera zilizokwenye uwanja kudukuliwa kwani kunaweza sababisha ajali. Kampuni iliyotengeneza teknolojia hiyo imehakikisha mfumo mzima unakuwa unajitegemea na upo salama, na pia waya za fiber za mawasiliano katika ya kiwanja cha ndege na ofisi iliyo umbali wa zaidi ya kilomita 100 zitakuwa tatu. Moja itakuwa ndiyo kuu na itakuwa inatumika na nyaya zingine mbili zitakuwa za ‘backup’ ili kusaidia kama hitilafu itatokea kwenye waya wa mawasiliano wa kwanza.
Teknolojia hiyo imetengenezwa na kampuni ya Saab Digital Air Traffic Solutions ya nchini Sweden na imefanyiwa majaribio ya kiusalama na ubora kwa miaka 10.
Ajira je?
Uongozi wa shirika la huduma za ndege nchini humo umesema hakuna atakayepoteza kazi katika kitengo hicho. Wafanyakazi wote watapatiwa mafunzo zaidi ya jinsi ya kutumia teknolojia hiyo mpya.