LG ni moja ya makampuni nguli ya muda mrefu zaidi katika sekta ya vifaa vya elektroniki. Na baada ya miaka mingi ya kitengo chake cha simu kufanya vibaya kimauzo sasa kimerudi kwenye mafanikio.
LG Electronics ni kampuni ya nchini Korea Kusini, ilianzishwa mwaka 1958
Miaka ya mwanzoni ya simu janja (smartphones) simu za LG zilibeba sifa za ubora na upekee wa hali ya juu tuu, ila inaonekana ushindani ulivyozidi kukua katika sekta hii kuna makosa yalifanyika na wakajikuta kitengo hicho cha biashara mauzo yake kushuka na kufikia hali ya kutengeneza hasara.
Mwaka wote wa 2016 kitengo hicho kilitengeneza hasara lakini katika miezi mitatu ya mwanzo wa mwaka huu kitengo hicho kimetengeneza faida.
Kampuni ya LG Electronics inaamini mafanikio yao yamechangiwa na toleo lao la simu ya LG G6 pamoja na zingine kadhaa zinazolenga watumiaji wa aina zote.
Kumekuwa na ukuaji mkubwa wa idadi ya simu walizoingiza sokoni – waliingiza simu milioni 14.8, ambao ni ukuaji wa asilimia 10 (wa mwaka hadi mwaka). Wakiwa na mauzo ya takribani dola bilioni 5.12 (Zaidi ya Trilioni 11.4 za Kitanzania) ambao ni ukuaji wa asilimia 8.8. Faida nyingi ikiwa imetokana na mauzo nchini Marekani.
Soma uchambuzi wa simu ya LG G6 – Simu ya LG G6: LG waonesha bado wapo makini na biashara ya simu