Mshauri wa mambo ya usalama wa Rais wa Marekani Donald Trump, Thomas ‘Tom’ Bossert amesema kwamba baada ya uchunguzi makini wamegundua kirusi cha WannaCry kimetokana na serikali ya nchi ya Korea Kaskazini.
Bwana Tom Bossert ameyasema hayo kupitia jarida la Wall Street linaloandika mambo ya kiteknolojia na kwamba madai yao yametokana na utafiti walioufanya na ushahidi walionao.
Hata hivyo hakuweka wazi ni ushahidi upi walio nao unaowatia hatiani Korea Kaskazini ila Whaite house itatoa maelezo zaidi ya ushahidi.
Malalamiko kama hayo yaliwahi kutolewa na Serikali ya Uingereza na kampuni ya Microsoft hapo awali kwamba kirusi cha WannaCry kinahusika na serikali ya Korea Kaskazini.
Kampuni ya Microsoft pia iliilaumu NAS kwa uzembe wa kuibiwa moja ya programu yake iliyosababisha kutengenezwa kwa kirusi cha WannaCry na kufanya mashambulizi ya kimtandao.
Kutolewa kwa taarifa hiyo kutaongeza mvutano kati ya nchi hizo mbili ambao zimekuwa zikivutana kuhusiana na silaha za nyuklia kwa muda mrefu kiasi cha kutishana kuingia kwenye vita.
Mwezi Mei mwaka huu kompyuta zinazotumia mfumo endeshi wa Microsoft zilishambuliwa na kirusi cha WannaCry na kusababisha huduma kadhaa kusimama. Aidha washambuliaji hao kupitia WannaCry walihitaji kulipwa kiasi cha fedha ili kuachia kompyuta walizoshambulia.