Data mpya zilizowekwa wazi na shirika linalofuatilia data mbalimbali, International Data Corp, zinaonesha mauzo ya simu janja yashuka barani Afrika katika robo ya kwanza mwaka huu ukilinganisha na kipindi cha robo ya mwisho ya mwaka jana.
Data hizo zinaonesha kulikuwa na jumla ya simu milioni 54.4 zilizoingizwa sokoni katika kipindi cha miezi mitatu ya mwaka huu (featured & smartphones – simu za kawaida na simu janja), hii ni asilimia 8.2 chini ukilinganisha na kipindi cha miezi mitatu ya mwisho wa mwaka jana.
Asilimia 40 ya simu janja zote zilizoletwa barani Afrika ni za bei ya chini ya dola 80 – takribani Tsh 160,000/= – IDC.
Ubaya ni kwamba katika simu janja, idadi ilishuka zaidi – asilimia 17.6, kutoka simu janja milioni 25.8 hadi milioni 21.2.
Hii inaonesha bado soko la simu za kawaida (featured phones ambazo huwa zinakuwa uwezo muhimu wa kupiga na kupokea simu, pamoja na kutuma ujumbe mfupi) bado lipo juu sana.
Afrika Mashariki bado soko linafanya vizuri
Kuporomoka kwa soko hilo kumechangiwa zaidi na uporomokaji wa idadi nzima ya simu janja zilizoingizwa kwenye mataifa yenye masoko matatu makubwa zaidi ya simu janja. Mzigo mzima wa simu janja zilizoingizwa nchini Afrika Kusini uliporoka kwa asilimia 13.6, huku Naijeria napo mzigo ulikuwa nchini kwa asilimia 8.1 na Misri chini asilimia 11.5.
Hali ilikuwa tofauti zaidi Afrika Mashariki ambapo kulikuwa na ukuaji wa mzigo mzima wa simu janja zilizoingia – hakuna eneo lingine la barani Afrika kulikuwa na ukuaji kama Afrika Mashariki.
Ukuaji huo ulichangiwa zaidi na Uganda na Tanzania, ambapo Uganda kulikuwa na ukuaji wa asilimia 11.6 na Tanzania ukuaji wa asilimia 8.1 wa idadi nzima ya simu janja zilizoingizwa ukilinganisha na kipindi cha robo tatu ya mwisho wa mwaka jana.
Samsung inaongoza barani Afrika kwa mauzo ya simu janja
Samsung ameendelea kuwa namba moja kwenye soko la simu janja Afrika, anamiliki soko kwa asilimia 29.8 katika kipindi cha miezi mitatu ya kwanza ya mwaka 2017. Baada ya Samsung ni Transsion Group wamiliki wa Tecno na Itel ambapo wana asilimia 23.4. Ila Transsion imefanikiwa zaidi kutokana na kuwa na simu janja za bei nafuu zaidi ukilinganisha na Samsung.
Chanzo: IDC na mitandao mbalimbali
One Comment
Comments are closed.