Andy Rubin, mmoja wa waanzilishi wa programu endeshaji ya Android amesema rasmi tayari anakuja na kampuni ya utengenezaji simu na simu yao ya kwanza itashindana rasmi na simu za ubora wa hali ya juu kama vile iPhone.
Bwana Andy Rubin alikuwa pia kiongozi wa kitengo cha Android katika kampuni ya Google na aliacha rasmi kazi mwaka 2014, akawa kimya sana kabla ya taarifa hizi mpya kutoka.
Android ilitengenezwa na kampuni ya Android Inc, ambayo Bwana Andy Rubin alikuwa mmoja wa waanzilishi. Mwezi Julai mwaka 2005 Google waliinunua Android Inc na kufanya Android kuwa moja ya kitengo chake, baada ya hapo ndipo historia ya simu zinazotumia Android ndio ilianza.
Kampuni mpya ya Bwana Rubin itafahamika kwa jina la Essential na inategemewa muda wowote kuanzia sasa atatangazwa rasmi kama Mkurugenzi mkuu, yaani CEO.
Kulingana na tovuti ya Bloomberg inategemewa Essential itakuja na simu janaj na vifaa janja vya majumbani. Lengo kubwa la Essential ni kuja na bidhaa za ubora wa juu kuweza kushindana na viwango vya iPhone 7, Samsung Galaxy S7, Google Pixel, na simu zingine za ubora wa juu zaidi.
Simu yao ya kwanza inategemewa kutambulishwa rasmi katika nusu ya pili ya mwaka huu na tayari wapo katika mazungumzo na kampuni nguli katika utengenezaji vifaa vya simu janja ya Foxconn inayotumiwa pia na Apple.
Soko la simu janja lina ushindani mkali sana. Essential kuweza kufanikiwa wanatakiwa kuleta bidhaa yenye utofauti wa hali juu ila kwa mtu ambaye amekuwa Google kwa miaka kadhaa kuna uwezekano mkubwa wakafanikiwa kuleta simu yenye mvuto sana.
Je unadhani inawezekana kwa kampuni nyingine kuweza kushindana na Samsung, Apple na Google kwenye eneo la simu janja za hadhi za juu?
Tuambie kwenye comment.
Kumbuka kusambaza makala na pia kuungana nasi kupitia Facebook, Twitter, Instagram, YouTube, Telegram na Google Plus
Vyanzo: theVerge na tovuti mbalimbali