Kwa mujibu wa EcoWatch India imeingia katika chati za nchi ambazo zina uzalishaji mkubwa wa umeme wa jua baada ya kuwasha mradi wake mkubwa wa umeme wa jua.
Mradi wa umeme kwa nguvu za jua wa Kamuthi unaopatikana katika jimbo la Tamil Nadu kusini mwa India uliwashwa mwezi wa tisa na kuiweka India katika ramani.
Mradi huu mpya ni mkubwa kiasi gani?
Mradi huu wa nguvu za jua unauwezo wa kufua kiasi cha Megawatts 648 wakati eneo ambalo mradi huu unachukua ni karibu heka 2500. Mradi huu baada ya kuwashwa uliupita mradi wa umeme wa jua ulipo Morocco na kuwa mradi mkubwa zaidi duniani ambao umefungwa katika sehemu moja.
Nini kimeihamasisha India kutekeleza mradi huu?!
India ni moja kati ya nchi zinazoendelea ambazo zimekumbwa na tatizo la uchafuzi wa mazingira uliokithiri, siku za hivi karibuni jiji la Delhi limeshuhudia viwango vikubwa vya uchafuzi wa hewa ambavyo vilipelekea mashule na shughuri za uzalishaji kusimama, hii imekuwa ni changamoto ambayo inailazimisha nchi hiyo ya bara la Asia kuongeza jitihada zake katika nishati mbadala.
India imekuwa na mpango madhubuti juu ya nishati mbadala ambazo ni rafiki na mazingira, mwaka 2014 waziri mkuu wa nchi hiyo Bw Modi alitangaza mpango wa kuongeza uwezo wa Solar wa india kufikia 100 Gigawatts hapo 2022.
Je Tanzania inasimama wapi katika umeme wa nguvu za jua?!
Nchi kama Tanzania ipo katika eneo ambalo linapata jua kwa wingi sana kwa mwaka na kama tutaamua kujikita katika kuvuna nishati hii basi tutaweza kuzalisha kiasi kikubwa cha umeme. Kwa sasa Tanzania haipo hata katika orodha ya nchi 50 bora zenye uwezo wa solar.