Msichana (Jina limehifadhiwa) wa Urusi katika jiji la Moscow mwenye umri wa miaka 13 amenusurika kifo alipoangukia waya za umeme kutoka kwenye daraja la reli wakati alipokuwa akijipiga selfie.
Picha zilizochapishwa na mashirika ya habari zilionyesha msichana huyo akining’inia kwenye waya za umeme.
Maafisa wa serikali walinukuliwa kusema kwamba msichana huyo alikuwa akirudi nyumbani na marafiki wake ndipo alipoamua kwenda pembeni mwa daraja kujipiga selfie wakati treni ya kusafirisha mizigo ilipokuwa ikikaribia, lakini kwa bahati mbaya akaanguka.
Wasamaria wema walimkimbiza hospitalini kwani alikuwa ameungua katika sehemu mbalimbali za mwili wake ikiwemo mkononi, mabegani na mguu wa kushoto.
Kulingana na ripoti za habari, mpita njia alitumia kamba kumvuta kumrudisha darajani huku wanakijiji wengine wakishikilia zulia kubwa chini yake endapo angeanguka.