Kwa takribani siku 3 za wiki iliyopita baadhi ya wateja wa mtandao wa Smile unaotoa huduma za intaneti kupitia teknolojia ya 4G LTE walijikuta kwenye wakati mgumu baada ya huduma ya intaneti kusumbua kwa wengi.
Kutokana na hali ya ushindani wa kwenye soko na vyanzo kadhaa kueleza ya kwamba mtandao huo upo kwenye hatihati ya kuondoka nchini, wiki hii tulipata nafasi ya kuzungumza na uongozi wa kampuni hiyo na kufahamu kiundani hali iliyotokea.
Wateja wengi wa Smile katika mikoa ya Mwanza, Arusha na baadhi ya maeneo ya jijini Dar es Salaam waliathirika kati ya Jumatano jioni (Tarehe 9 Agosti) hadi huduma iliporejea tena siku ya Jumamosi asubuhi (13 Agosti).
Kwa ufupi ni kwamba mtandao huo ulipata hitilafu za kimitambo, na kupitia mazungumzo yetu na Meneja Uhusiano wa kampuni hiyo tumefahamu haya yafuatayo kuhusu tatizo hilo.
- Tatizo lilikuwa la kiufundi, liliathiri watumiaji wengi ila si wote.
- Wakati wote tatizo lilipokuwa linaendelea walikuwa wanajitahidi kuwakifia wateja wao wote kwa sms mara kwa mara kuwaomba msamaha na kuwapa taarifa juu ya tatizo la huduma.
- Timu yao inapitia taarifa za wateja walioathirika na kuwapatia ofa ya thamani ya upotevu wa huduma waliyoipata.
Ingawa mtandao wa TheExchange uliandika na tukaunukuu juu ya kufungwa matawi/ofisi zao kadhaa maeneo ya jiji la Dar es Salaam, wao wamekanusha hilo. Na tayari wameanza kuchukua hatua kadhaa kuwasiliana na TheExchange kuhusu taarifa hiyo (hadi sasa bado hawajafanikiwa kuwafikia).